Wanaume 7 kati ya 10 wana michepuko

Muktasari:

  • “Akijiamini kuwa sisikii alipanga mipango ya kukutana na mwanamke ambaye baadaye nilimfahamu kuwa niliwahi kufanya naye kazi kampuni moja kabla ya kuacha na kufungua biashara zangu,” anaanza kusimulia Christina Christopher mkazi wa Mbagala jijini Dar es Salaam.

“Nimemsikia kila alichokuwa anapanga kufanya siku inayofuata, baada ya kuzungumza kwenye simu akiamini nimelala kwa sababu nilikuwa naumwa na nilipewa dawa nilizopewa ni za usingizi aliamini siyasikii maongezi yale.”

“Akijiamini kuwa sisikii alipanga mipango ya kukutana na mwanamke ambaye baadaye nilimfahamu kuwa niliwahi kufanya naye kazi kampuni moja kabla ya kuacha na kufungua biashara zangu,” anaanza kusimulia Christina Christopher mkazi wa Mbagala jijini Dar es Salaam.

Mwanamke huyu anasema, kusikia habari hizo ni kujiridhisha lakini kwa miaka mingi alihisi kuwa na ‘wasaidizi’ kutokana mwenendo wa mume wake.

Anasema amedumu kwenye ndoa hiyo kwa miaka 22 sasa, kutokana na kumuacha kama alivyo lakini kadri wanavyozeeka ndivyo mumewe anavyozidi kujipambanua wazi kuwa ana wanawake nje.

Utafiti wa kisaikolojia uliofanywa na mwandishi Christopher Ryan, mwaka 2010 na kuchapishwa katika kitabu kiitwacho Sex at Dawn: The Prehistoric Origins of Modern Sexuality, kimebaini kuwa asilimia 63 ya wanaume na asilimia 45 ya wanawake wamewahi kuwa na uhusiano nje ya ndoa zaidi ya mara moja.

Utafiti mwingine Truth About Cheating uliochapishwa mwaka 2014, kuhusiana na usaliti katika ndoa ulibaini kuwa zaidi ya asilimia 40 ya ndoa huvunjika kabla ya kutimiza miaka 30 kutokana na wanaume kuwa na uhusiano nje ya ndoa zao.

Utafiti uliolenga kubaini sababu za wanaume kutoka nje ya ndoa, ilifanywa na mshauri wa masuala ya saikolojia na mwandishi, Dk Gary Neuman uliohusisha watu 200 katika nchi mbalimbali kupitia mitandao ya kijamii na kubaini ongezeko la wanaume wanaotoka nje ya ndoa zao.

Utafiti huo ulibainisha asilimia 48 ya wanaume hawaridhishwi na huduma ya mapenzi wanayopewa na wake zao, kitu kinachowafanya watafute huduma hiyo nje.

Dk Neuman alisema tamaduni zinaonyesha kuwa sababu kuu za furaha ya mwanaume ni pamoja na kukatwa kiu ya mapenzi, huku wakiendeshwa zaidi na hamu ya kufanya mapenzi kuliko wanawake jambo ambalo huwawia vigumu kuzuia tamaa zao za kimwili.

Utafiti huo unaonyesha kuwa licha ya wanaume kusukumwa kufanya mapenzi bado hawana ujasiri wa kueleza hisia zao mara nyingi kwa wake zao.

“Wanawake wanaweza kufanya jambo moja tu kukomesha tabia hii, nalo ni kuonyesha wameridhika na mapenzi wanayopata hata kama hawajaridhika, kutafuta namna ya kukataa kujamiiana badala ya kukataa moja kwa moja,” anasema Dk Neuman.

Utafiti huo ulibaini kuwa asilimia 66 ya wanaume karibu katika nchi zote alizopata maoni walijisikia vibaya kutoka nje ya ndoa zao.

Ulifafanua kuwa asilimia 68 ya waliotoka nje ya ndoa hawakupanga kufanya hivyo na wanajutia kitendo hicho.

“Wanaume wana uwezo wa kujipanga kwa ajili ya kukutana na wapenzi wao hata baada ya mwezi mmoja, hivyo katika ndoa kila mmoja ana wajibu wa kuwa mlinzi wa mwenzake kwa sababu anaweza kuapa hatafanya na akafanya hivyo baadaye,” alishauri Dk Neuman.

Ilibainika pia asilimia 77 ya wanaume walitoka nje ya ndoa kutokana na kitendo hicho kufanywa na rafiki zao.

Dk Neuman alisema wanaume wengi hujiridhisha kuwa jambo hilo kama limefanywa na rafiki zao hakuna neno na wao wakifanya.

Akizungumzia hali hiyo mtaalamu wa saikolojia, Modesta Kamongi anasema kutoka nje ya ndoa kwa wanaume ni rahisi kutokana na kuwa na nafasi kubwa ya kuzunguka na marafiki kuliko wanawake.

Anasema wanaume wengi hufanya hivyo siyo kwa kupenda bali kutokana na wanachokiona kwa marafiki zao.

“Ukumbuke tangu enzi mwanaume mwenye wanawake wengi ndiyo alikuwa anasifiwa, isipokuwa tofauti ya sasa na wakati ule wao walifanya rasmi kwa kuoa wake hata 10.

“Kwa utamaduni huo mwanaume anajiona hana thamani wala jina mbele ya wenzake kama hana kimada, hivyo kisaikolojia mwanaume aliye na kimada hujiamini mbele ya wenzake na kujivuna,” anasema Kamongi.

Dk Neuman anaunga mkono kilichosemwa na Kamongi kwa kueleza kuwa utafiti wake ulibaini wanaume hupata kishawishi cha kutoka nje ya ndoa kulingana na marafiki wanaokutana nao wakiwa matembezini.

Anayataja maeneo hatari kwa wanaume kukutana na wanawake kwa kufuata mkumbo kuwa ni baa, klabu, hotelini wakati wa chakula cha mchana na katika viwanja vya michezo.

Kamongi anasema kisaikolojia ni ngumu mwanaume kumuepuka mwanamke anayeonyesha dalili na mitego ya kumtaka, ukilinganisha na wanawake.

Anasema hata kama atamuepuka ni baada ya kutoka naye mara moja ama mbili na hilo pia hutokana na tamaduni zilizopo kuwa mwanaume rijali hatakiwi kumuogopa mwanamke zaidi ya kutoka naye.

Hilo nalo limejitokeza katika utafiti wa Dk Neuman na asilimia 40 ya wanaume wanaotoka nje ya ndoa hukutana na wanawake kazini, huku wengi wa wanawake hao wakitumia mbinu mbalimbali kuwatega.

“Maswali kama unapenda mwanamke wa aina gani, unajisikia huru kutoka na mke, hujitokeza wakati wa kujadili miradi mbalimbali na hata wafanyakazi wa jinsi mbili tofauti wanapokuwa safarini kikazi,” alisema Neuman.

Dk Neuman anawashauri wanawake kuhakikisha wanazifanya ndoa zao zinabaki katika mapenzi kama ilivyokuwa wakati wanakutana.

Alifafanua kuwa alichobaini katika utafiti ni asilimia 12 ya wanaume wanafurahia mapenzi moto ikiwamo kuvutiwa zaidi na maumbile ya wanawake.

Alisema asilimia hiyo pia walikiri kufurahishwa zaidi na mapenzi ya wasaidizi wao wa kazi kuliko wake zao.

“Sababu kuu ni wakifika kwa wasaidizi wanapata mapenzi tofauti na yanayovutia kutokana na kuwa na vitu vipya na wanaume siku zote hupenda kuona vitu vipya vinavyowahusu wanawake ndiyo maana hubadili hata maeneo ya kupata kinywaji baada ya kazi ili kuona vitu ambavyo hawajaviona katika maeneo waliyozoea,” alisema Neuman.

Utafiti huo uliochapishwa kwa mara ya kwanza mwaka 2015 ulibaini kuwa asilimia sita ya wanaume wanaotoka nje ya ndoa walikutana na wanawake na kwenda nao faragha muda mchache baada ya kukutana.

Alisema ni asilimia 73 ya wanaume hujitahidi kuwazoea wanawake wanaokutana nao kwa muda wa zaidi ya mwezi kabla ya kwenda nao faragha.

“Wanawake wanaweza kuona dalili za mwanaume anayemfuatilia mwanamke ikiwamo kuchelewa kurudi nyumbani, kutodai unyumba, malumbano yasiyokuwa na sababu ya msingi na kukataa kupokea simu zako,” alisema Neuman.

Kitabu cha nne cha mshauri wa ndoa na mtunzi, Esther Perel kiitwacho “Cheating in the Age of Transparency”, kimeeleza kuwa wanaume wana uwezo mkubwa wa kuwa na uhusiano zaidi ya mmoja ukiachilia ndoa zao.

Takwimu za kuvunjika ndoa

Asilimia 17 ya ndoa zilizovunjika sababu wanandoa kutokuwa waaminifu katika ndoa zao.

Asilimia 70 ya wanaume waliooa walikubali kuwa wanawasaliti wake zao kwa kuwa na uhusiano zaidi ya mmoja nje ya ndoa.

Tafiti nyingine zinabainisha kuwa asilimia mbili ya tatu ya wanawake hawafahamu kuwa wame zao wana uhusiano nje ya ndoa. Utafiti huo uliochapishwa kwa mara ya pili mwaka 2015 umeonyesha kuwa idadi ya wanaume wanaosaliti ndoa zao inaongezeka kila siku huku nyingi zikishindwa kufikisha miaka 25 kutokana na usaliti.

Kilichonishangaza hata baada ya kumfumania na kufahamu kuwa ana wanawake zaidi ya wawili tofauti na mimi alisisitiza kuwa ananipenda.

Anasema siyo tu kunipenda bali kutokuwa na furaha iwapo tutaachana kama ambavyo mimi nilikuwa nataka.

“Misamaha ilikuwa sehemu ya ndoa yetu, nikimsamehe kwa kubaini ana kimada huyu baada ya miezi mitatu namkamata na ujumbe mwingine wa mapenzi, unaoashiria walikuwa jana faragha, wanapanga kwenda au kusafiri wakale raha nje ya nchi.

“Nikasikia sauti ya malalamiko ya shutuma nje ya chumba chetu, nikatuliza akili, nikabaini ni mume wangu,” anasema.

“Nilichokisikia baada ya hapo sikutaka kuamini, kutokana na majibu yake inaonekana kuna mwanamke alikuwa na uhusiano naye amemfumania na mwanamke mwingine hivyo anabembeleza asiachwe.

Kauli yake ya mwisho ni “Kama umeng’ang’ania tuachane kwa kosa nisilolifanya basi bwana, kila ninalokueleza huniamini umeng’ang’ania hunitaki basi nashika ustaarabu wangu.

Anasema baada ya malumbano hayo mumewe alirudi ndani na akajifanya alikuwa amelala ameshtuliwa na ujio huo.

Alipojaribu kumshika na kumuuliza jambo alikuwa mbogo asiyetaka usumbufu na kujibu kwa ukali “Nipe nafasi ya kutafakari basi”.

Anasimulia akajiridhisha kuwa mumewe ameachika kwa sababu ya kufumaniwa, ina maana ndani ya ndoa ana uhusiano na wanawake wawili tofauti waliojimilikisha kama mume wao.

Kisa hiki cha mama Lugano kama alivyopenda kuitwa ni kimoja lakini vipo vingi vya aina hiyo ambavyo huchangia kwa kiasi kikubwa kuvunja ndoa.

Tafiti mbalimbali zinaonyesha wanaume walioko ndani ya ndoa wana uhusiano zaidi ya mmoja nje.