Wapo kina Rayvanny wengi tu tatizo ni kukariri

Muktasari:

Wapo wapi kina Grace Matata, Vumilia, Beka, Hard Man na wengine? Muziki umewatema au kutokuthubutu kumewaweka benchi.

Siyo mashabiki na wadau waliokariri kuwa wanamuziki wanaoweza kufanya makubwa ni Diamond, Alikiba na labda Vanessa Mdee kwa mbali, hata wasanii wenyewe wanaamini hivyo.  Naamini hivyo kwa sababu hata kujaribu wamewaachia wao.

Wasanii wanaogopa kujaribu kushiriki wakiamini level hizo ni za wasanii fulani na wao hawahusiki kabisa. Wanaamini wanaandika nyimbo wapate shoo tu basi.

Wenye vipaji kama Rayvanny wapo wengi lakini vinaishia wapi? Hawa wanaojiita viongozi wanachoangalia ni kuingiza fedha lakini siyo kujaribu kupanua wigo kwa kushiriki tuzo za Kimataifa.

Wapo wapi kina Grace Matata, Vumilia, Beka, Hard Man na wengine? Muziki umewatema au kutokuthubutu kumewaweka benchi.

Zamani tuzo za Channel O ilikuwa dili yaani ukisikia msanii fulani amewahi kushinda unaona ni kitu kikubwa. Lakini mtoto kutoka Tandale, Diamond ndani ya usiku mmoja alizinyakua tatu. Hii inaonyesha kumbe hata sisi tunaweza sema basi tu uthubutu umekuwa butu.

AY pia amewahi kushinda tuzo ya Channelo O. Siyo tuzo za Channel O tu, MTV zipo nyumbani. Diamond amewahi kushinda tuzo za MTV Base na EMA. Alikiba kadhalka. Vannesa Mdee amewahi kushinda tuzo za Afrimma ambazo hutolewa kila mwaka nchini Nigeria.

Tuzo ya BET ni kubwa ambayo kwa Afrika Mashariki tuna ukame naye. Ukiitaja tuzo hiyo kwa Afrika Mashariki mbele yake litakuwapo jina la msanii wa Uganda, Eddy Kenzo.

Mwaka jana mwanamitindo Millen Magese aliitwaa tuzo ya BET kwa mchango wake kwa jamii katika kuielemisha kuhusiana na ugonjwa wa Endomitriosis.

Ushindi wa Rayvanny sio miujiza. Imetokana na uthubutu labda wa msanii mwenyewe au uongozi unaosimamia kazi zake.

Wasanii wenye vipaji sawa na Rayvanny au kumzidi wapo wengi lakini kinachowakwamisha ni hali ya kukariri kuwa wapo kina fulani wa kufanya hivyo.

Wapo ambao wamekaririshwa kuwa Diamond huwa anahonga ili ashinde tuzo. Kama hilo lingekuwa linawezekana angehonga aishinde hii maana ni kama imegoma kabisa kutua mikononi mwaka.

Mwaka jana tulishuhudia Black Coffee akimtoa kapa Diamond kwa kuinyakua. Kama angeipata sasa angekuwa anasubiri ya Grammy tu kuweka rekodi ya dunia kwa sababu tuzo kubwa zote angekuwa ameshazitwaa.

Rayvanny awafungue kuwa hakuna bahati wala uchawi katika mambo haya. Ni kujituma na kufanya kazi kwa bidii. Kina Rayvanny wapo wengi tu sema hawajiamini.