Wasanii waanze kujifunza kuweka na kurekebisha taarifa mitandaoni

Muktasari:

Miongoni mwa mambo mengi yanayowaangusha wasanii ni namna ya kutojua kutumia majukwaa mengine ili waendelee kudumu katika kazi ya sanaa. Wanamuziki wanaamini akisharekodi wimbo na kutoa video kazi imeisha.

Wasanii wakubwa huwa wanachukua hatua pale anapoona mtandao au chombo cha habari kimetoa taarifa inayopotosha uhalisia.

Huwa wanalazimisha ziondolewe au marekebisho yafanyike. Huku ni kujijenga. Sina hakika na alichokifanya Benpol hivi karibuni kwa kuweka picha yake akiwa mtupu kama kinamjenga.

Miongoni mwa mambo mengi yanayowaangusha wasanii ni namna ya kutojua kutumia majukwaa mengine ili waendelee kudumu katika kazi ya sanaa. Wanamuziki wanaamini akisharekodi wimbo na kutoa video kazi imeisha.

Akimaliza kurekodi wimbo na video atazunguka katika vituo vya redio na televisheni kufanya promo baada ya hapo atakaa chini akisubiri mialiko ya matamasha.

Wanasahau kuwa majukwaa ya kujitangaza ni mengi na kila moja lina mbinu zake. Mbaya zaidi hawataki kujifunza au kujiuliza kwa nini fulani amefikia hapo.

Ukifuatilia kwa ukaribu hasa katika magazeti utaona wasanii wanaoandikwa ni wale wale kila siku na huenda unajiuliza inakuwaje hili linatokea.

Ukweli ni kuwa wasanii hawa ndiyo wale wanaofahamu umuhimu wa kuandikwa, iwe kwa uzuri au ubaya.  Hivi Kim Kardashian au Paris Hilton unaweza kuwaeleza tofauti ya kuandikwa kwa uzuri na ubaya? Umezuka mtindo hapa nchini pia wa wasanii kujitengenezea matukio mabaya au kutunga stori mbaya kuwahusu ili wazungumziwe.  Hapa ndiyo utakubaliana nami kuwa kuandikwa kwa mabaya au mazuri kote kuna faida.

Wapo wasanii ambao hawajui kutumia nafasi na pia ni kitu ambacho hakipo katika programu zao za kila siku. Kwa mfano msanii hajui umuhimu wa kutumia mitandao ya kijamii au gazeti kujikuza kisanii.

Wasanii wanaoandikwa ni walewale kila siku kwa kuwa ndio wanaopatikana na pia picha zao zinapatikana kwa urahisi. Unaweza kutafuta taarifa za msanii fulani kwenye mitandao au picha bila mafanikio.

Taarifa za msanii na picha vinapopatikana kwa urahisi ndivyo visababishi vikuu vya kuona wanaoandikwa ni walewale kila siku ndani na nje ya nchi.

Wasanii wanaotoa nyimbo nzuri na video ni walewale, mwisho wa siku huonekana wanabebwa lakini juhudi zao zinawafanya waonekane kila kukicha. Wajifunze kuwa ili uwe msanii ni lazima ukamilike kila idara. Kama taarifa zako zinatafutwa kwa tochi wewe ni ‘underground’.