Yuko akademi Marekani lakini ndoto yake ni Taifa Stars

Muktasari:

Na Spoti Mikiki imechangia kuonyesha baadhi ya wachezaji walio nje, hasa Hamis Abdallah (Sony Sugar),Abdul Hilal (Tusker) na Aman Kyata (Chemelil) za Kenya ambao wameanza kuitwa kulitumikia taifa lao kwenye kikosi cha timu ya Taifa.

jambo ambalo linaweza kuwa linamrahisishia kazi kocha wa Taifa Stars, Salum Mayanga utayari wa wachezaji wanaosakata soka nje ya nchi kuja kulitumikia taifa lao.

Na Spoti Mikiki imechangia kuonyesha baadhi ya wachezaji walio nje, hasa Hamis Abdallah (Sony Sugar),Abdul Hilal (Tusker) na Aman Kyata (Chemelil) za Kenya ambao wameanza kuitwa kulitumikia taifa lao kwenye kikosi cha timu ya Taifa.

Wiki iliyopita tuliona safari ya Yusuf Juma ambaye anaichezea Monroe SC, tangu ilivyoanzia mkoani Kigoma hadi Marekani ambako nako yuko mbioni kuondoka kutokana na kuhitaji sana kwake kucheza barani Ulaya akizipigia hesabu Arsenal na Chelsea.

Wiki hii tunaye mdogo wake, Abdallah Juma (16) ambaye yupo kwenye kituo cha New England Revolution akipatiwa misingi ya mpira kabla ya kuanza kucheza soka la ushindani.

Abdallah anakaribia kutimiza miaka 16 hivi karibuni ameongea na gazeti hili kutoka kwenye kambi ya kituo hicho iliyopo Florida, Marekani na kusema japo amekulia Marekani lakini anatamani kuanza kuzichezea timu za vijana za nchi yake ya Tanzania.

“Kucheza timu za vijana kuna umuhimu wake, inategemea na mipango ya makocha husika ambao nadhani wamekuwa wakiita wachezaji kutokana na mahitaji yao, nipo kwenye hiki kituo ila natamani kuzichezea timu za vijana za Tanzania.

“Nilitoka Tanzania na kuja huku Marekani na familia yangu nikiwa mdogo sana, sina kumbukumbu nyingi kuhusu nchi yangu ila ninachojua, mimi ni Mtanzania, kukulia kwangu Marekani hakunifanyi niwe na uamuzi wa kuwa raia wa huku.

“Ndoto yangu ni kuwa mchezaji mkubwa ili nilisaidie pia Taifa langu la Tanzania kwenye ngazi tofauti za timu za Taifa,hata kama ikitokea nimeshawishiwa kuachana na Tanzania na kuichezea Marekani sintokuwa tayari,” anasema Abdallah.

Ameendelea.”Ujinga ni kuisaliti nchi yako, hakuna sababu ya kunifanya niisaliti Tanzania na natamani sana siku nikipata nafasi nirudi ili nilione vizuri Taifa langu, maana nasikia kwanza lina vivutio vingi vya Utalii,”

Abdallah ambaye anamudu kucheza kwenye nafasi ya kiungo mshambuliaji, amesema namna soka la kufundishwa linavyoweza kumfanya mchezaji kuwa bora zaidi.

“Kila siku tunausoma mpira ambao unamambo mengi, sio kuucheza tu uwanjani, mchezaji kwenye kituo chochote cha soka huwa anaandaliwa kuja kuwa mchezaji wa kulipwa hivyo kuna vitu vya ziada anavipata ikiwemo kucheza kwa nidhamu.

“Ukikizoea kitu basi utakuwa unakifanya kwa umakini, kadri unavyosisitiziwa nidhamu na kuifanyia kazi kila siku inakujenga mchezaji, sio nidhamu pekee pia kuna mbinu mbalimbali za mpira na mengineyo mengi ambayo mchezaji binafsi anatakiwa kuwa nayo.

“Mwenye kipaji halisia akiongezea na maarifa ya kwenye kituo cha mpira basi ni wazi huyo mchezaji atakuwa na uwezo mara mbili, yule ambaye anakipaji na hata hajapitia kwenye kituo atakuwa na uwezo mara moja labla kipaji chake kiwe cha hali ya juu,” anasema.

Mdogo huyo wa Yusuf,amesema kuwa anasimamiwa na kaka yake hivyo suala la wapi anategemea kucheza kama akipevuka kwenye kituo hicho alishindwa kutoa jibu la moja kwa moja na mwishowe kumsukumia Hamis ambaye ni kaka yake mkubwa.

“Kaka Hamis ndiyo anaweza kuzungumzia hilo vizuri, nipo kwenye hiki kituo yeye ndiye anafanya mipango nje ya kutusimamia pamoja na kaka yangu mwingine Yusuf hivyo siwezi kulizungumzia hilo sana.

“Ila natamani zaidi kucheza Ulaya, soka la Ulaya linamvuto zaidi na hata ushindani wake ni mkubwa kama utalinganisha na huku,” anasema kiungo huyo mchezeshaji.

Hamis, akimzungumzia mdogo wake, Abdallah anaeleza namna ambavyo anaweza kumudu kuwasimamia wadogo zake pamoja na mipango yake kwa ujumla ilivyo.

“Soko la mpira wa Ulaya linalipa hivyo nimeopanga kujikita zaidi na Ulaya, Yusuf nimeshafanya mpango kwa kuzungumza na timu kadhaa ambazo atakwenda kufanya majaribio mwenzi,Januari.

“Abdallah yupo kwenye kituo sina haraka naye maana anamuda wa kuendelea kujifunza, atakapomaliza mafunzo yake tutaangalia ni wapi patakuwa sehemu sahihi kwake, kinachonipa faraja ni kuwa wote wawili wanauwezo mkubwa.

“Kama misingi ya mpira wanayo kwa hiyo hata kwenye kufanya majaribio hawawezi kukwama kabisa kwa kukosa timu za kuzichezea, kikubwa tuombe uzima,” anasema kaka huyo.