Ligi ya RBA kuanza kutimua vumbi Gymkhana
Muktasari:
- Kocha wa Oilers, Lusekelo Nbweled ametamba kuwa wamejiandaa kucheza kwa umoja kuanzia kwenye kujilinda hadi wakati wa kushambulia.
Dar es Salaam. Ligi ya Mpira wa Kikapu (RBA) hatua ya robo fainali itaanza kutimua vumbi kesho Ijumaa kwa JKT kucheza na ABC, Oilers itaanza na Pazi kwenye Uwanja wa Gymkhana, Posta.
Kocha wa Oilers, Lusekelo Nbweled ametamba kuwa wamejiandaa kucheza kwa umoja kuanzia kwenye kujilinda hadi wakati wa kushambulia.
“Solomon atakosekana kutokana na tatizo lake la goti, wengine wote wapo fiti, upamoja wetu wa kiuchezaji lazima utatusaidia na tutahakikisha hatutoi nafasi ya kucheza upande wetu,” alisema Lusekelo.
Naye mshauri wa ufundi wa Pazi, Mpoki Mwakipake amesema kuwa timu yao imejitahidi kufanyia kazi maeneo muhimu ambayo yalionekana kuwa na upungufu.
Michezo hiyo ya robo fainali itachezwa kwa mfumo wa mikondo mitatu ya kila mchezo ambao utachezwa na mshindi wa jumla atapata nafasi ya kwenda hatua ya nusu fainali.