Muktasari:

Nyota huyo wa tenisi Marekani amekuwa katika mahusiano kwa miezi 15 na mchumba wake Alexis Ohanian mmiliki wa Reddit waliochumbiana Desemba mwaka jana.

Serena mjamzito wa wiki 20.
New York, Marekani
Serena Williams ametumia mtandao wa Snapchat kuiambia dunia kuwa ni mwenye ujauzito wa wiki 20.

Nyota huyo wa tenisi Marekani amekuwa katika mahusiano kwa miezi 15 na mchumba wake Alexis Ohanian mmiliki wa Reddit waliochumbiana Desemba mwaka jana.

Serena ( 35) alitegemea kurejea katika namba moja ya ubora wa tenisi wiki ijayo, lakini kwa hali yake ya sasa itamlazimisha kukaa nje ya uwanja kwa msimu mzima pamoja na kukosa mashindano ya Wimbledon.

Hiyo inamaanisha kwamba atashindwa kutetea taji lake la Wimbledon alilotwaa mwaka jana baada ya kumshinda Angelique Kerber kwa seti 7-5, 6-3.

Pia, inaonyesha kwamba Serena alikuwa mjamzito wakati aliposhinda taji la 23 la Grand Slam la mashindano ya Australian Open mwezi Januari mwaka huu.

Serena ambaye wiki ijayo atakuwa mchezaji namba moja, atabaki katika nafasi yake kwa mujibu wa sheria WTA, kama atakuwa tayari kurejea uwanjani na kushiriki mashindano ndani ya miezi 12 baada ya kujifunga.

Hata hivyo, picha yake hiyo aliiondoa haraka mtandao, lakini wawakilishi wake baadaye walithibisha ujauzito huo.

Waandaji wa mashindano ya tenisi ya US Open walimpogeza: “Imekuwa ni siku ya furaha kwetu na Serena Williams kwa kuingia katika dunia mpya! Hongera kwa kutegemea kupata mtoto hivi karibuni!”