Malinzi, Mwesigwa wapigwa kalenda tena

Dar es Salaam. Rais wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Jamal Malinzi amerejeshwa rumande kwa wiki nyingine mbili baada ya kesi inayomkabili ya kugushi nyaraka na kutakatisha fedha kushindwa kuanza kusikilizwa kutokana na upepezi kutokamilika.

Malinzi anayetuhumiwa na mashtaka 28 tofauti pamoja na Katibu Mkuu wa TFF, Celestine Mwesigwa na Mtunza Fedha, Nsiande Mwanga wanaokabiliwa na mashtaka matatu, wamepandishwa kwenye Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu leo Jumatatu asubuhi, chini ya Hakimu Mkazi Mkuu, Willbroad Mashauri, lakini kesi hiyo haikuweza kusikilizwa.

Mawakili wa upande wa Jamhuri ambao ndiyo walalamikaji, waliiambia Mahakama kwamba upelelezi wa kesi hiyo bado haujakamilika, hivyo washtakiwa hao kurejeshwa rumande hadi Julai 31.

Awali, Malinzi na wenzake walisomewa mashtaka hayo ya kughushi nyaraka na kutakatisha fedha, Juni 29 mwaka huu, na kupelekwa rumande kutokana na kesi hiyo kutokuwa na dhamana na sasa wataendelea kusubiri kwa wiki hizo mbili.