Okwi, Bocco wamuibua straika Mnenge Suluja

Masoud Masasi,Mwananchi [email protected]

Mwanza.Mchezaji wa zamani wa Simba, Mnenge Suluja amemtaka kocha Pierre Lechantre kusaka mshambuliaji mwenye kiwango bora kama Emmanuel Okwi na John Bocco.

Suluja alisema Lechantre anatakiwa kupata mchezaji mwenye uwezo mzuri wa kufunga mabao kama Okwi au Bocco.

Okwi, mchezaji wa kimataifa wa Uganda, amefunga mabao 20 na Bocco 14 katika Ligi Kuu Tanzania Bara. Alisema Simba imekuwa ikipata taabu ya kufunga mabao Okwi au Bocco wanapokuwa nje ya uwanja kutokana na majeraha au dharura.

Alisema Simba inaweza kuyumba endapo Okwi na Bocco watakosekana katika mechi za mashindano ya kimataifa. Simba inatarajiwa kushiriki Ligi ya Mabingwa Afrika.

“Simba inatakiwa kusajili washambuliaji wenye uwezo wa kufunga kwa sababu akikosekana Bocco au Okwi timu haiko sawa,”alisema Suluja.

Hata hivyo, Suluja alisema Simba imefanya kazi nzuri msimu huu kwa kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu Tanzania Bara waliokosa kwa miaka mitano.