VIDEO: AliKiba akinukisha Mkwakwani, Coastal Union yashikwa Mbeya City

Muktasari:

  • Hii ni mechi ya kwanza kwa Kiba kupangwa katika kikosi cha kwanza cha Coastal Union tangu alipojiunga nayo mwanzo wa msimu huu.

Tanga. Mwanamuziki na mshambuliaji wa Coastal Union, Ali Kiba amekonga nyoyo za mashabiki wa timu yake kwa kucheza dakika 64, na kusababisha bao katika sare 1-1 dhidi ya Mbeya City kwenye Uwanja wa Mkwakwani, Tanga.
Kiba tangu aliposajili wa Coastal alikuwa hajaichezea timu hiyo kwa sababu mbalimbali lakini leo alianza katika kikosi akiwa mshambuliaji 10, amevalia jezi yake namba 7.
Katika mchezo huo mashabiki wengi waliojitokeza uwanjani hao walishudia uwezo mzuri wa kujituma wa Kiba katika dakika 5, alipata mpira na kupiga shuti lililogonga beki wa Mbeya City na kuwa kona iliyopigwa na Athuman Idd ‘Chuji’ na kumkuta Ayoub Rouben alifunga bao la kuongoza kwa wenyeji.
Shangwe hiyo ya Coastal Union ilidumu hadi mapumziko wakati Mbeya City iliposawazisha dakika 48, baada ya beki Bakari Mwamnyeto kujifunga mwenye wakati akijaribu kuokoa krosii iliyochongwa na Eliud Ambokile.
Katika dakika 62, Kiba alipata mpira akiwa katika eneo la 18 na kupiga shuti la chini lililodakwa na kipa Mbeya City, dakika mbili baadaye kocha Juma Mgunda kumtoa na nafasi yake kuchukuliwa na Deogratius Anthony.
Awali Kiba aliingia uwanja hapo akiwa na gari yake binafsi aina ya Mercedes Benz na kuungana na wachezaji wenzake wa Coastal Union.
Hata hivyo tofauti na ilivyotarajiwa na wengi kuwa Kiba angekuwa katika basi lililobeba wachezaji wote wa Coastal Union, hali ilikuwa tofauti.
Wachezaji wote wa Coastal wakiwa wanashuka kwenye gari hiyo mchezaji Ally Kiba hakuonekana baada ya muda mfupi alionekana akiwasili uwanjani hapo akiwa na gari yake.
Kiba alifika uwanjani hapo akiwa na gari yake aina ya Mercedes Benz ambayo kabla ya kushuka mbele na nyuma kulionekana kuwa na walinzi wakimlinda na kumuelekeza kwa kuiweka gari.
Mara baada ya kuiweka gari alishuka akiwa amevaa jezi namba saba huku akishika vifaa vyake vingine mkononi kama viatu, jezi na vingine.
Mapema timu ya Mbeya City ilikuwa ya kwanza kuwasili katika uwanja wa CCM Mkwakwani Tanga kwa ajili ya mechi na Coastal Unioni ambao walikuwa wa pili kuwasili uwanjani hapo wakiwa na gari yao aina ya Coaster.