Azam yamuunganisha Mudathir na Pluijm

Muktasari:

Azam inafanya mchakato wa kumnasa beki wa pembeni ili kuiimarisha safu yao ya ulinzi.

Dar es Salaam, Mudathir Yahya, aliyekuwa anakipiga Singida United amesaini mkatabawa miaka miwili na klabu yake ya Azam FC na sasa anajiandaa kwa ajili ya msimu ujao wa ligi kuu akiwa na Wanalambalamba hao.

Mudathir ambaye anacheza nafasi ya kiungo, awali Azam ilimtoa kwa mkopo kwenda Singida United chini ya kocha Mholanzi Hans Pluijm. Akiwa na kikosi hicho cha Singida, Mudathir alicheza kwa kiwango cha juu na kuisaidia kumaliza kwenye nafasi ya tano. 

Usajili wake ndani ya Azam ni kama amerudi nyumbani kwa mara nyingine na sasa atakuwa pamoja na Pluijm aliyechukua mikoba ya Aristica Cioaba.

Ni usajili mwingine baada ya Mzimbabwe  Tafadzwa Kutinyu pamoja na Kocha Hans Pluijm kutoka Singida United. Na imekuwa rahisi kwa Mudathir kurudi Azam kutokana na namna Pluijm anavyomfahamu vizuri mchezaji huyo na sasa wameelekeza nguvu zao kusaka beki wa pembeni ili kuimarisha safu ya ulinzi.