Bingwa Ligi Kuu enzi hizo yapambana na hali yake

Muktasari:

Klabu hiyo kwa sasa inaoongoza kundi A lenye timu sita na imekuwa ya kwanza kati ya makundi manne ya ligi hiyo.

Rungwe. Klabu ya Tukuyu Stars ambayo imewahi kunyakua ubingwa wa Ligi Kuu Tanzania Bara mwaka 1986 ‘Banyambala’ ya mjini Tukuyu-Rungwe imetangulia hatua ya hatua sita bora katika ligi daraja la tatu ngazi ya mkoa inayoendelea kutimua vumbi katika viwanja tofauti mkoani hapa.

Juzi, Tukuyu Stars ilikuwa na kibarua kizito dhidi ya Bagamoyo FC ya zote za mjini Tukuyu na kufanikiwa kuichapa bao 1-0, mechi iliyochezwa kwenye Uwanja wa Tandale mjini Tukuyu.

Bao pekee la Tukuyu Stars liliwekwa wavuni na mchezaji Dorian Mwamakimbuka dakika ya 80, bao lililodumu hadi dakika ya 90 ya mchezo huo.

Stars imefikisha pointi 10 kwa mechi zake tano ilizocheza kwenye hatua ya makundi na kufanikiwa kushinda mechi tatu kutoa sare moja pamoja na kufungwa mechi moja.

Kocha Mkuu wa Tukuyu Star, Alex Mwambipile alisema ni jambo la kheri kwa timu yake kufanikiwa kushika nafasi ya kwanza na kutangulia katika hatua ya awali ya timu sita zitakazopambana ili kupata bingwa wa mkoa.