Cannavaro augua ghafla kambini

Muktasari:

  • Cannavaro alifanya mazoezi ya Jumatatu na juzi Jumanne lakini jana alijisikia vibaya na kuwahishwa hospitali ya jirani ili kutazamwa afya yake.

Njombe. Nahodha wa Yanga, Nadir Haroub "Cannavaro" amelazimika kukosa mazoezi ya jana Jumatano jioni baada ya kuugua ghafla akiwa kambini.

Cannavaro alifanya mazoezi ya Jumatatu na juzi Jumanne lakini jana alijisikia vibaya na kuwahishwa hospitali ya jirani ili kutazamwa afya yake.

Nahodha huyo alipelekwa na daktari wa timu, Edward Bavu lakini hakukutwa na tatizo lolote hivyo kushauriwa apate mapumziko.

"Sijakutwa na Malaria kama tulivyodhani, nimeambiwa ni uchovu tu hivyo nikapumzike," alisema Cannavaro.

Yanga leo Alhamisi itasafiri kwenda Songea tayari kwa mchezo dhidi ya Majimaji unaotarajiwa kufanyika Jumamosi.