DB Queens mabingwa kikapu wanawake RBA

Muktasari:

  • Akizungumza baada ya kumalizika mchezo huo, uliofanyika kwenye Uwanja wa Ndani ya Taifa, Dar es Salaam, shujaa wa timu hiyo Jesca Julius aliyefunga vikapu 20 peke yake katika mchezo huo, alisema kuwa uzoefu ndio uliowaangusha.

Dar es Salaam. Timu ya Ukonga Queens imejitetea kuwa imepoteza mchezo wa fainali ya ubingwa wa kikapu wa RBA 2018 kwa wanawake kutokana na kukosa uzoefu.

Akizungumza baada ya kumalizika mchezo huo, uliofanyika kwenye Uwanja wa Ndani ya Taifa, Dar es Salaam, shujaa wa timu hiyo Jesca Julius aliyefunga vikapu 20 peke yake katika mchezo huo, alisema kuwa uzoefu ndio uliowaangusha.

“Kwa kweli ni kukosa uzoefu tu tuliwaachia wapinzani wetu wakapata pointi nyingi katika robo ya kwanza hadi sisi tunazinduka wenzetu wakawa wameshajiweka vizuri.

“Pamoja na yote, kikubwa ninawapongeza wachezaji na viongozi wote wa Ukonga kwa hatua tuliyofikia, wameonyesha kwenye wana kitu katika mchezo huu wa kikapu,” alisema.

Katika mchezo huo, DB Queens ikiwatumia wachezaji wake mahiri Maria Mabela aliyefunga pointi 18 na Lamana Peter aliyefunga 17, imetwaa ubingwa wa RBA 2018 kwa wanawake baada kuichapa Ukonga Queens kwa vikapu 76-57.

Mchezo huo fainali uliokuwa mkali na kusisimua, washindi walianza kuongoza tangu filimbi ya kwanza, walimaliza robo ya kwanza wakiongoza kwa vikapu 10-0.

Ukonga Queens walianza kuzinduka katika robo ya pili na kuonyesha upinzani wa hali ya juu baada ya nyota wake Jesca Julius na Noela Lwandaman kuonyesha uwezo mkubwa wakifunga vikapu 15 lakini wakati huo sasa, DB Lioness walikuwa wamefikisha vikapu 19.

Vijana wa Ukonga walishangaza wengi kwa kuonyesha uwezo mkubwa na kutawala kabisa robo ya pili kiasi kwamba hadi robo ya pili inamalizika Ukonga Queens walipindua matokeo na kuongoza kwa vikapu 29 kwa 28.

Katika robo ya tatu, DB Lioness walizinduka na kuwapeleka puta wapinzani hao na hadi inamalizika walikuwa mbele kwa vikapu 45 huku Ukonga Queen wakiwa na vikapu 40 huku.

Ukonga Queens walionekana kukata pumzi katika robo ya mwisho na kuwapa mwanya DB Lioness kujiongezea vikapu wakiwatumia vizuri wachezaji wao waliokuwa warefu kusaka ushindi.

Hadi mchezo huo unamalizika DB Queens walitoka kifua mbele wakivuna vikapu 76 na kutangazwa mabingwa, huku Ukonga Queens wakipongezwa kwa kushika nafasi ya pili licha ya kwamba ndiyo wanacheza fainali yao ya kwanza ya Ligi hiyo iliyojizolea umaarufu mkubwa.