Kipanga akaribia Stand United

Muktasari:

Stand United ina pointi sita walizozipata baada ya kucheza mechi 10, ndiyo inashika mkia kwenye msimamo wa ligi kuu.

MSHAMBULIAJI wa JKT Ruvu, Sady Kipanga huenda akasaini mkataba wa mwaka mmoja na klabu ya Stand United kwenye dirisha dogo la usajili msimu huu.

Kipanga ambaye kwa mwonekano ni mrefu, anatakiwa na klabu hiyo kwa ajili ya kuokoa jahazi la Stand ambalo linaweza kuzama wakati wowote kutokana na kuwepo katika nafasi mbaya ya kushuka daraja.

Mmoja wa viongozi wa Stand United ambaye hakutaka jina lake litajwe alisema,  wameanza usajili na  wachezaji wanaowafikilia ndani ya kikosi chao ni wale wazoefu ili waiokoe timu hiyo ibaki ligi kuu.

Stand yenye pointi sita tu walizozipata baada ya kucheza mechi 10, ndiyo inaburuza mkia kwenye msimamo wa wa ligi kuu.