Lechantre asuka upya jeshi Simba

Muktasari:

  • Simba inasaka ubingwa wa kwanza wa Ligi Kuu baada ya kukaa miaka minne bila ya kutwaa taji hilo

Kocha Mfaransa wa Simba, Pierre Lechantre amesema mazoezi wanayofanya sasa ni kuhakikisha wanashinda katika mchezo wao ujao wa Ligi Kuu Bara dhidi ya Njombe Mji.

Kikosi cha Simba kilifanya mazoezi leo asubuhi kwenye Uwanja wa Boko Veterans  walianza mazoezi ya kupasha misuli na viungo, baada ya kumaliza mazoezi hayo ya viungo walipangiwa koni aina tano tofauti na waligawana katika makundi na kila kundi lilikuwa na wachezaji watatu.

Mazoezi hayo yalikuwa ya nguvu mno kwani Lechantre akisaidiana na wasaidizi wake Masoud Djuma na kocha wa viungo Mohammed Habib walikuwa wakali na kutaka kila mchezaji afanye kwa ufasaha.

Lechantre alisema mazoezi haya yatatusaidia katika mechi yetu ya Njombe Mji kwani uwanja wanaotumia hauruhusu mchezaji kukaa na mpira kwa muda mwingi, lakini mazingira ya uwanja huo yanahitaji wachezaji kutumia nguvu zaidi.

"Baada ya hapa tutafanya mazoezi ya kupasia na kupokea haraka mpira huku tunaenda mbele na kubwa sitapenda kuona mchezaji anakaa na mpira kwa muda mrefu," alisema Lechantre.

Mfaransa huyo alisema wachezaji wengine wa kikosi cha kwanza wapo katika majukumu ya timu zao za taifa na nimegundua hawa niliobaki nao hawana ufiti wa kutosha ndio maana tunafanya mazoezi haya.

"Wachezaji wengi niliobaki nao huwa hawapati nafasi ya kucheza mara kwa mara na nimeona hawana ufiti wa kutosha, lakini nataka kuuongeza kwa wale ambao nao wamepata nafasi ya kucheza," alisema.