Lechantre kuwafanyia 'surprise' mastaa Simba

Muktasari:

  • Zawadi hizo zinazotambulika kama MO Simba Awards, zinafanyika kwa mara ya kwanza katika kikosi hiko.

Dar es Salaam, Kocha wa Simba Mfaransa Pierre Lechantre ambaye aliwaacha wachezaji wake katika mashindano ya SportPesa nchini Kenya kabla ya kumalizika leo Jumatatu jioni atafanya jambo moja la kushtukiza sana.

Lechantre amepanga kuibuka katika hafla ya Simba ambayo itakuwa ni kwa ajili ya ugawaji tuzo itakayofanyika kwenye Hoteli ya Kilimanjaro na shughuli nzima itaanza saa 11.

Tuzo hizo zitahusisha sehemu mbalimbali kama benchi la ufundi, mchezaji bora wa msimu, beki bora, kiungo bora, mashambuliaji bora, shabiki bora na nyingine.

Lechantre ambaye atafahamu hatma yake kesho Jumanne kama ataendelea kubaki Simba kwa ajili ya msimu ujao au ataondoka, atawepo katika hafla hiyo kama kocha mkuu na atapokea tuzo kama kawaida.

"Nitakuwepo pale na wachezaji wangu pamoja na viongozi katika kusheherekea siku muhimu kama hii kwani itakuwa siku ya kipekee kwa kuwa wachezaji na viongozi tunaagana wengine wanakwenda likizo na wengine ndiyo ikawa basi," amesema Lechantre.

Mara baada ya shughuli hizo kumalizika kocha wa viungo wa Simba, Mohammed Habib atakwenda kwao Tunisia kwa mapumnziko na Lechantre hatma yake ni baada ya makubaliano ya mwisho.

Zawadi hizo zinazotambulika kama MO Simba Awards zinafanyika kwa mara ya kwanza katika kikosi hiko.