Habibu Kondo: Tumekuja kuifunga Yanga siyo kutalii

Muktasari:

  • Mchezo wa Yanga na Majimaji unatarajiwa kuchezwa kesho Jumatano kwenye Uwanja qwa Uhuru.

KOCHA wa Majimaji ya Songea, Habibu Kondo anasema amekuja kuchukua pointi tatu dhidi ya Yanga na siyo kutalii kama wengi wanavyowachukuliwa kwamba ni wakufungwa.

Kondo amekiri kwamba mechi itakuwa ngumu, lakini hawana budi kupambana ili kuondoa kasumba ya kuona timu za mikoani ni kwa ajili ya kufungwa Yanga na Simba.

"Mechi itakuwa ngumu, ila tumekuja kuandika historia ya kuchukua pointi tatu Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam, ifahamike hatujaja kutalii na kurejea tulikotoka,"anasema.

Kondo anasema kikosi chake kipo imara kwa ajili ya kazi na kina morali ya kutosha kwa ajili ya mchezo huo,hivyo anawaomba wenye mapenzi na Majimaji wajitokeze kwa ajili ya kuwaunga mkono.

"Mashabiki wa Majimaji popote walipo wajitokeze kwa ajili ya kutuunga mkono ili tuweze kufikia lengo kushinda mechi hii,tunajua ngumu ila tutapambana kadri tuwezavyo ili tupate pointi tatu,"anasema.