Julio aisuka upya Dodoma FC

Muktasari:

Dodoma FC inapambana kupanda Ligi Kuu Bara kwa mara ya kwanza msimu huu

Dodoma. Mshambuliaji wa zamani wa Simba, Shija Mkina amesaini maktaba wa kuicheza Dodoma FC.

Usajili wa Mkina aliyewahi kung’ara akiwa na Simba umekuwa ni usajili mkubwa wa Dodoma Fc inayosaka kupanda daraja msimu huu.

Akizungumzia usajili wa Mkina pamoja na nyota wengine akiwemo Magadula na Frank Sekule, kocha Jamhuri Kiwhelo ‘Julio’ alisema wameangalia uzoefu wa wachezaji hao wanaamini utawabeba kwenye mechi zilizobaki za lala salama.

“Mechi zilizobaki ni za kupigana kufa ua kupona ndio maana tunawasajili wachezaji wenye uzoefu wa kupambana na bila shaka Mkina, Magadula na Sekule tunategemea watatusaidia kwenye mbio zetu za kwenda Ligi Kuu mwakani,” alisema Julio.

Wakati huohuo; Chama cha soka mkoani Dodoma {Dorefa} kimetangaza kuanza kwa mchakato wa ligi ya mkoa kwa usajili wa wachezaji uliofunguliwa Desemba 4 hadi Desemba 22.

Tofauti na msimu uliopita kulikuwa na vituo 4 vya ligi hiyo safari hii ligi ya mkoa itafanyika kwenye vituo viwili pekee ambavyo ni Kibaigwa na Kondoa Mjini wakati 8 bora itachezwa mjini Dodoma.