Watano tu wacheza dakika 810 Mtibwa

Muktasari:

Wachezaji hao walitumika kwa dakika zote kutokana na mahitaji ya timu kwa kuchezi dakika zote katika mechi tisa.

WACHEZAJI watano ndani ya kikosi cha Mtibwa Sugar, wamepiga bao la maana  baada ya kucheza dakika zote 810 katika mechi tisa, tangu msimu wa ligi kuu ulipoanza.

Wakali hao ambao ni pamoja na Dickson Daud, Casian Ponela, Issa Rashid 'Baba Ubaya, Shaaban Nditi na Mohamed Issa 'Mo'.

Kocha mkuu wa Mtibwa Sugar, Zubery Katwila ambaye anafurahia kiwango cha wachezaji wake amesema, wachezaji hao walitumika kwa dakika zote kutokana na mahitaji ya timu.

"Kwa ujumla Mtibwa ya mwaka huu, najivunia kuwa na aina ya wachezaji nilionao, kila mmoja anajituma kutokana na majukumu yake uwanjani na ndiyo maana tunafanya vizuri,"alisema Katwila.

"Hiyo ndiyo iliyopelekea hata hao watano Dick, Ponela, Issa, Nditi na Mo wacheze dakika zote 810."

Kikosi cha Mtibwa ambacho mchezo ujao,  kitacheza na ndugu zao Kagera Sugar, kama kawaida yao wanapokuwa mwanzoni mwa msimu huwa hawakamatiki, kinashika nafasi ya nne na pointi 17 sawa na Yanga iliyo ya tatu, ya pili ni Azam FC ina pointi 19 sawa na vinara wa ligi klabu ya Simba.