Prisons sasa kugawa dozi tu
Muktasari:
Prisons ambayo mchezo uliopita ilitoka sare ya mabao 2-2 na Majimaji, Jumamosi itacheza na Ndanda kwenye Uwanja wa Sokoine Mbeya.
Dar es Salaam. Kocha Mkuu wa Prisons, Abdallah Mohammed amesema wameyafanyia kazi makosa yaliyojitokeza katika mchezo dhidi ya Majimaji wiki iliyopita na sasa wako tayari kuikabili Ndanda Jumamosi
Prisons ambayo mchezo uliopita ilitoka sare ya mabao 2-2 na Majimaji, Jumamosi itacheza na Ndanda kwenye Uwanja wa Sokoine Mbeya.
Mohammed ambaye pia aliwahi kuinoa Ndanda anakutaka na waajiri wake wa zamani huku akijiamini kuwa ataibuka na ushindi dhidi yao licha ya kwamba Ndanda walipata ushindi wa bao 1-0 dhidi ya wapinzani wao wakubwa Mbeya City Jumapili iliyopita.
"Tumejipanga vizuri kwa mchezo huo, najua Ndanda ni timu nzuri lakini timu yangu ni nzuri zaidi, hivyo tunawangoja kwani hatutakubali tufanye tena makosa kama tuliyofanya mchezo uliopita kwa sababu tunajua mchezo wa mpira si kitu cha kuaminika dakika zote 90.
"Kwenye mchezo uliopita dhidi ya Majimaji tulicheza vizuri lakii baadaye tulifanya makosa na kuwatafutia goli lililofanya tugawane pointi. Sasa hatutaki yatokeee hayo dhidi ya Ndanda," alisema Mohammed.
Prisons imeanza vizuri Ligi Kuu Bara msimu huu baada ya mechi ya kwanza kuifunga Njombe Mji ugenini kwa bao 1-0 kabla ya kutoka sare ya mabao 2-2 nyumbani dhidi ya Majimaji ya Songea.