Simba, Yanga macho yote Cairo

Muktasari:

  • Mwaka huu Yanga iliondoshwa raundi ya kwanza na Zanaco baada ya kutoka nao sare ya 1-1 nyumbani kabla ya kulazimishwa suluhu ugenini na Wazambia kufuzu kwa faida ya bao la ugenini.

SIMBA na Yanga zinaendelea kupiga tizi kwenye viwanja viwili tofauti, Yanga wakiwa Uwanja wa Uhuru, wakati wakati zao Simba wapo kambi ya jeshi, Chuo cha Polisi KUrasini, lakini akili na macho yao yote yapo Cairo nchini Misri.

Klabu hizo zinaelekeza macho yao huko kwa kuwa, droo ya mechi za awali na zile za raundi ya kwanza inafanyika leo jijini humo ambapo itafahamika wazi  wawakilishi wetu watapangwa na klabu zipi katika mechi hizo za mchujo.

Simba inarejea kwa mara ya kwanza kwenye mechi za kimataifa tangu mwaka 2013 ikishiriki Kombe la Shirikisho Afrika na Yanga itacheza tena Ligi ya Mabingwa Afrika mwakani.

Droo hiyo inatarajiwa kufanyika mchana huu na itafahamika wawakilishi wetu hao na wale wa visiwani Zanzibar, JKU na Zimamoto wataanzia wapi dhidi ya nani katika kusaka tiketi ya kuingia hatua ya makundi kusaka mamilioni ya CAF.