Simba yafa kishujaa Zambia, Mtibwa Sugar hoi

Muktasari:

  • Licha ya Simba kupoteza mchezo huo imejiweka katika mazingira mazuri baada ya kufunga bao la kufutia machozi dakika ya 73. Matokeo ya 2-1 yamewapa ahueni kwenye mechi ijayo ya marudiano ambapo wanahitajika kushinda bao moja tu.

Timu ya Nkana Rangers ya Zambia imeibuka na ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Simba mchezo uliopigwa leo Jumamosi kwenye Uwanja wa Nkana, Kitwe nchini Zambia.

Mabao ya Nkana yaliwekwa wavuni na Donald Kampamba (26') na Kelvin Kampamba (56') na kuwafanya mashabiki wa timu hiyo kuzidisha hamasa ya kuwashangilia wachezaji wao uwanjani.

Simba ilikwenda mapumziko ikiwa nyuma ya bao moja lakini hata hivyo kipindi cha pili walirejea kwa kusuasua hali iliyosababisha dakika tano za mwanzo Nkana kutawala mchezo huo.

Dakika ya 56 Nkana walijikuta wakiwainua mashabiki wao kupitia kwa Kelvin ambapo  dakika ya 73 Simba ilipata bao kwa mkwaju wa penalti kupitia kwa John Bocco.

Kipa wa Simba, Aishi Manura alijkuta akiruhusu bao la mapema kutokana  na kukosa umakini langoni huku wapinzani wao wakitumia makosa hayo.

Simba wanawasubiri Nkana kwenye mchezo unaofuta wa marudiano na unatarajiwa kuchezwa kwenye Uwanja wa Taifa wiki ijayo.

Wakati wawakilishi hao wa Ligi ya Mabingwa wakipoteza mchezo huo, Mtibwa Sugar wamepoteza mchezo wao Kombe la Shirikisho baada ya kukubali kipigo cha mabao 3-0 ugenini nchini Uganda dhidi ya KCCA.