Stand United yamrejesha kocha Bilo

Muktasari:

  •  Kocha huyo amekuwa na timu hiyo kwa zaidi ya misimu miwili kabla ya kusimamisha mwishoni mwa mwaka jana

Mwanza.Stand United imemrejesha kikosini kocha wake msaidizi Athumani Bilali “Bilo” aliyesimamishwa kwa utovu wa nidhamu takribani miezi miwili iliyopita.

Katibu Mkuu wa Stand United, Kennedy Nyangi amethibitisha kurejeshwa kikosini kwa kocha huyo na tayari ameanza kazi rasmi.

“Alisimamishwa kwa utovu wa nidhamu, lakini badaaye kamati tendaji iligundua tuhuma zilizokuwa zinamkabili hazikuwa na ukweli tumeamua arudi aendelee na kazi yake,” alisema Nyangi.

Kocha Bilo alisema tayari yupo kwenye kambi ya timu hiyo alianza kazi rasmi ya kukinoa kikosi hicho.

Alisema anawashukuru viongozi wa timu hiyo kwa kumrejesha ndani ya timu na sasa atahakikisha Stand United inatoka mkiani kwenye msimamo wa Ligi Kuu.

“Nimerejea kikosini na hivi ninapozungumza na wewe (mwandishi) hapa nipo mazoezi ujio wangu nitahakikisha timu inatoka huku mkiani,”alisema Bilo.

Kocha huyo alijitapa kuwa ataanza kazi rasmi katika mchezo wao wa Ligi Kuu dhidi ya Ruvu Shooting utakaopigwa Jumamosi ya wiki hii mjini Shinyanga.

“Nitaanza kazi rasmi na Ruvu Shooting ninawaambia mashabiki watulie mambo mazuri yanakuja kamwe hatuwezi kushuka Daraja msimu ujao”alisema Kocha huyo.