Tambwe: Bado nipo nipo sana Yanga

Muktasari:

Mshambuliaji huyo baada ya kusumbuliwa na majeruhi kwa muda mrefu ameanza kurejea na tayari amefunga mabao manne

Dar es Salaam. Mshambuliaji Mrundi Amis Tambwe amesema hana mpango wa kuondoka Yanga kwa sasa pamoja na mkataba wake kuelekea mwishoni.

Tambwe na kiungo Thaban Kamusoko wanahusishwa na kutaka kuachwa na Yanga kutokana na umri wao kwenda na kusajili nyota wengine kabla ya kufungwa kwa dirisha la usajili Desemba 15.

Akizungumzia taarifa za kuachwa kwake Tambwe amesema amekuwa akizisikia katika vyombo vya habari, lakini uongozi wake hujawahi kumtamkia wala kumuandikia barua hivyo ataendelea kukitumikia kiksi hicho.

Tambwe alisema ni kweli mkataba wake unamruhusu kufanya mazungumzo na klabu nyingine, lakini hana mpango huo kwani bado anaamini ananafasi ya kuendelea kuitumikia klabu hiyo.

"Dirisha la usajili litafungwa Disemba 15 bado sijapata ofa kutoka kwa timu yoyote na wala sijazungumza na Yanga kuhusiana na kuongeza mkataba mpya, lakini ninachoweza kukwambia ni kwamba bado nipo nipo Yanga," alisema Tambwe mwenye mabao manne katika Ligi Kuu.