Uongozi Nyanza wacharuka watimua kocha, wachezaji

Muktasari:

  • Nyanza yapoteza mechi nne mfululizo Ligi Daraja la Pili na hasira zatua kwa kocha, wachezaji.

MABOSI wa timu ya Nyanza FC iliyopo Ligi Daraja la Pili (SDL) imetangaza kumpiga chini Kocha Mkuu wao, Rashid Idd 'Chama' na kusimamisha wachezaji wao watatu kama njia ya kuiweka sawa timu yao inayoyumba katika ligi ya SDL.

Katibu Mkuu wa Nyanza, Daniel Ndaikya alisema wamemsimamisha Chama kwa sababu ya matokeo mabaya ya timu yao, lakini pia ni kwa kutoelewana na msaidizi wake.

“Tumepoteza mechi nne mfululizo katika SDL na kipigo cha 4-0 dhidi ya AFC Arusha ndio yanayotuuma hakuna anayefurahia timu kufanya vibaya sio kwa viongozi ama wanachama, hivyo tumeamua kumsimamisha kocha,” alisema Ndaikya aliyeongeza kuwa pia wamesimamisha nyota wao watatu.

Alisema wachezaji hao aliokataa kuwataja majina wamesimamishwa kwa kosa la utovu wa nidhamu

Hata hivyo, Ndaikya alikiri kuwepo kwa mgomo wa chini kwa chini unaofanywa na wachezaji wanaodai zaidi ya Shilingi 10 milioni za usajili na malipo mbalimbali za benchi la ufundi.