UCHAMBUZI: Mambo matatu Yanga wamesahau kwa Kakolanya

Muktasari:

  • Baada ya kujiondoa katika kikosi cha Yanga, wapenzi na Uongozi wa Yanga umeamua kusahau mazuri ya Kakolanya

Dar es Salaam. Kumeibuka maneno mengi baada ya kipa Beno Kakolanya kugoma kujiunga na wachezaji wenzake katika kikosi cha Yanga.

Kakolanya tangu atoke katika kikosi cha timu ya Taifa kilichotoka kucheza mechi dhidi ya Lesotho, hakurejea kwenye klabu yake kwa kile kinachotajwa kudai fedha yake ya usajili.

Hata hivyo inatajwa kwamba mara kwa mara alikuwa akiwakumbusha mabosi wake kuhusu kulipwa, lakini mabosi hao walikuwa wakimpotezea.

Mwanaspoti limeangazia baadhi ya vitu ambavyo Kakolanya alijitolea kwenye klabu hiyo licha ya kwamba alikuwa na madai yake.

 

KUCHEZA ANAUMWA

Msimu uliopita kipa Youthe Rostand aligoma kusafiri na timu kwenda mkoani Mbeya kucheza na Tanzania Prisons.

Kakolanya aliyekuwa majeruhi ya goti, alienda katika timu hiyo ili akae benchi tu, lakini alikutana na kisanga hicho na kujikuta akisafiri kama golikipa pekee.

Ilimlazimu kucheza huku akiwa na maumivu ya goti, akiwa anadai mishahara na pesa yake ya usajili lakini kwa mazingira yake aliona bora akae golini na kuisaidia timu yake, lakini leo uongozi wa Yanga umesahau kabisa.

Kama angekuwa na utovu wa nidhamu au jeuri angegoma kipindi kile, lakini Kakolanya alipambana lakini leo hii inabidi tutambue kwamba na yeye ni binadamu labda kapatwa na tatizo kubwa kwanini agome hivi sasa akiwa mzima na sio mwanzo alipopewa mechi huku anaumwa.

KUIPA YANGA UBINGWA

Msimu wa mwaka juzi alisajiliwa akitokea katika klabu ya Prisons, usajili ambao pia alihusishwa kujiunga na Simba, lakini akatua Yanga.

 

katika msimu huu kwenye mechi 5 za mwisho aliipambania Yanga akiwa golini mpaka wanafanikiwa kuchukua ubingwa.

Leo hii kisa kagoma wameanza kusema kwamba meneja wake ni Simba basi amegoma ili asajiliwe Simba, wakati huo huo wanasahau Kakolanya huyu alisaini Yanga na meneja huyo huyo na akainyima Simba ubingwa mwaka juzi.

MICHOMO YA SIMBA NA YANGA

Baada ya mechi ya Yanga dhidi ya Biashara kocha Mwinyi Zahera alifunguka anashangaa kuona meneja wa Beno ni mjumbe wa Simba.

Watu wa karibu na kocha huyo wanamlisha maneno sio kwa sababu Kakolanya huyu ambaye alidaka mechi dhidi ya Simba meneja wake ni huyo huyo mjumbe wa Simba.

Kama ingekuwa anafuata kauli za meneja wake asigeokoa michomo katika pambano hili, hivyo kudai kwake pesa kusiwafanye viongozi wa Yanga kusingizia mambo ya nje ya uwanja kwa kipa huyu.