Mbao sasa kukaza kupitiliza mechi za Simba, Yanga

Muktasari:

  • Kocha asisitiza kuwa udhamini mpya wa maji utawawezesha kukaza zaidi sio kwenye mechi wanapokutana na Simba na Yanga pekee.

Klabu ya Mbao FC imesema kuwa inaamini itafanya vizuri zaidi kwenye ligi kuu kutokana na sapoti inayoendelea kupata kutoka kwa wadau na makampuni mbalimbali.

Katibu Mkuu wa timu hiyo, Daniel Naila amesema kuwa Mbao lazima ifanye vizuri kutokana na jinsi inavyopata sapoti kutoka kwa wadau na makampuni na kusema kuwa malengo yao ni makubwa katika tasnia ya mpira nchini.

Amesema kuwa kitendo cha Kampuni ya Jambo Food Product kukubali kuwapatia maji kwa kipindi hiki cha msimu huu uliobaki, kinazidi kuwapa nguvu katika ushiriki wao wa ligi kuu.

"Niseme kwamba tutafanya vizuri na kufika mbali,lakini pia tunahitaji tena wadhamini kutuunga mkono ili kufikia malengo...huu ufadhili wa maji kutoka kwa kampuni ya Jambo Product ni chachu kwetu," amesema Naila.

 

Kwa upande wake Meneja Masoko wa kampuni ya Jambo Product, Johnson Mchuma amesema kuwa lengo lao kwa siku za usoni ni kuwa wadhamini wakuu wa timu hiyo.

 

Amesema kuwa licha ya kutoa maji kwa mechi zilizosalia kwa timu hiyo,bado kampuni itakuwa inatoa misaada nyingine ikiwamo mafuta kwa ajili ya safari.

 

"Mbali na maji kwa kila mechi watakazokuwa wanacheza popote,lakuni tutakuwa tunawasaidia misaada nyingine kama mafuta pale watakapokwama,kushirikiana nao kwenye shughuli za kijamii, lakini kubwa tunataka kuwapindua GF ambao ni wadhamini wao wakuu ili sisi (Jambo) ndio tuwe wadhamini wakuu" amesema Mchuma.

 

Ameongeza kuwa licha ya timu kufanya vizuri, lakini pia wamevutiwa na utendaji kazi mzuri wa uongozi (Katibu na Mwenyekiti)wa timu na kwamba watahakikisha wanatoa ushirikiano wa kutosha ili kusonga mbele.