Wanamichezo, wananchi kumuaga Bendera Jumamosi

Muktasari:

Bendera ambaye aliwahi pia kuwa Naibu Waziri wa Michezo, ndiye kocha pekee wa soka aliyewahi kuiongoza Taifa Stars kwenye Fainali za AFCON za 1980.

Dar es Salaam. Mwili wa aliyekuwa Mkuu wa Mkoa wa Manyara na kocha wa zamani wa Taifa Stars, Joel Bendera utaagwa Jumamosi kwenye Hospitali ya Lugalo kwa ajili ya mazishi yatakayofanyika Jumapili wilayani Korogwe.

Bendera alifariki jana Jumatano baada ya kuugua kwa muda mfupi.

Ndugu wa marehemu ambaye pia aliwahi kuwa Mwenyekiti wa Baraza la Michezo la Taifa (BMT), Kanali Iddi Kipingu alisema msiba kwa Dar es Salaam huko Sinza ambako pia kuna makazi yake.

"Taarifa zilizopo ni kwamba mwili wa mpendwa wetu asubuhi hii (Desemba 7) unatolewa Muhimbili kuhamishiwa Lugalo ambapo utaagwa Jumamosi na mazishi ni Jumapili," alisema Kipingu.