Wenger ampa Sanchez mshahara mnono

LONDON, ENGLAND. Kocha wa Arsenal, Arsene Wenger anaamini wazi Alexis Sanchez anabaki katika klabu hiyo  ili kukamilisha mipango yake ya kufanya kweli kwenye Ligi Kuu England msimu ujao.

Sanchez siku chache tu zilizopita aliripotiwa akidai anataka kucheza kwenye timu inayoshiriki Ligi ya Mabingwa Ulaya kwa sababu anataka kubeba taji hilo.

Wenger anafahamu makali ya Sanchez na ndiyo maana amepanga kumpa mshahara wa Pauni 275,000 kwa wiki ili asaini mkataba mpya wa kubaki hapo na asiende kujiunga na wapinzani wao kwenye Ligi Kuu England.

Hata hivyo, Sanchez mwenyewe anaripotiwa kutaka alipwe Pauni 300,000 kwa wiki, hivyo hapo kutakuwa na pungufu ya Pauni 25,000.

Ni wazi kabisa kama Arsenal itatangaza tu kumpiga bei Sanchez, basi timu wapinzani wao kwenye Ligi Kuu England kama Manchester City, Chelsea na Manchester United zitaingia kwenye vita ya kuisaka saini yake.

Kikosi cha Arsenal kwa sasa kipo huko Shanghai, China na Sanchez hayupo kwenye timu kwa sababu ameongezewa siku za kumpumzika kwa kuwa alikuwa kwenye mashindano ya Kombe la Shirikisho na atajiunga na timu yake Julai 30.