Wenger amtuliza Sanchez kilaini

Muktasari:

  • Klabu hizo zimekuwa katika mvutano mkali wa kutaka kuinasa saini ya mchezaji huyo ambaye amebakisha mkataba wake chini ya mwaka wa kuitumikia klabu hiyo.

 Kocha wa Arsenal, Arsene Wenger anakaribia kuzima ndoto za Manchester City na Paris Saint-Germain kuinasa saini ya mshambuliaji wake, Alexis Sanchez baada ya kuwepo taarifa kuwa mchezaji huyo amekubali kusaini mkataba mpya wa dau la Pauni300,000 kwa wiki.

Klabu hizo zimekuwa katika mvutano mkali wa kutaka kuinasa saini ya mchezaji huyo ambaye amebakisha mkataba wake chini ya mwaka wa kuitumikia klabu hiyo.

Kwa muda mrefu, mchezaji huyo amekuwa akidengua kumwaga wino Arsenal ambayo ilianza kumpa Pauni 225,000 kwa wiki akakataa na kuongeza pamoja na bonasi nyingine hadi kufikia Pauni275,000 lakini akazitolea nje vilevile.

Hata hivyo, pamoja na Sanchez kukataa fedha hizo, aliwaweka wazi kuwa anataka Pauni300,000 na inaelezwa kuwa klabu hiyo imekubali yaoishe na kukatisha tamaa klabu zilizokuwa zikimfukuzia.

Mchezaji huyo alisema  kuwa mpango wake ni kutaka kucheza London lakini katika klabu nyingine huku Wenger akigoma kumwachia.