Ile ishu ya Hawa wa Diamond bado kidogo

LICHA ya msanii wa Bongo Fleva, Naseeb Abdul ‘Diamond’ kumtaka Hawa achague biashara ya kufanya baada ya kumaliza matibabu, mama yake amesema bado binti yake hayupo vizuri na anahitaji kupumzika.

Mama mzazi wa Hawa, Ndagina Shabani, amesema binti yake ana jeraha kubwa la upasuaji aliofanyiwa kule India na anahitaji muda wa kupumzika kwa muda.

“Tumesikia msaada wa Diamond kwa mtoto wetu, tunazidi kushukuru kwani kama siyo yeye Hawa asingekuwa hivi leo, lakini kidonda bado na kitachukua hadi mwaka kupona.

“Hapa ana mshono na kwa kweli sikutarajia kama angenyanyuka wakati wa upasuaji ule, namshukuru Mungu na mwanangu Diamond kwa kuokoa maisha ya binti yangu, kama familia tulianza kukata tamaa kabisa.

Kutokana kutakiwa kukaa katika mazingira tulivu, mama huyo alisema Hawa anaishi hotelini na atakuwa huko kwa miezi mitatu.

Hawa, ambaye awali aligundulika kuwa ana tatizo kwenye ini na baadaye ikabainika ni moyo na siyo ini, aliondoka nchini Oktoba 18 kwenda India kwa matibabu na kurejea Novemba 20, mwaka huu.

Hawa ametamba kwenye ngoma ya Nitarejea ya Diamond iliyoachiwa mwaka 2011, ambayo alikuwa gumzo kinoma.