Miongoni mwa sababu zinazowafanya wanawake kushindwa kubeba ujauzito

Muktasari:

  • Hata hivyo, utafiti unaonyesha kuwa hivi sasa asilimia kubwa ya wanaume husumbuliwa na tatizo hilo bila wao kujijua.

Siku chache zilizopita nilieleza kuhusu sababu kubwa zinazowafanya wanaume wengi kupoteza uwezo wa kutungisha mimba hata kama nguvu zao za jinsi zipo sawa.

Hata hivyo, utafiti unaonyesha kuwa hivi sasa asilimia kubwa ya wanaume husumbuliwa na tatizo hilo bila wao kujijua.

Lakini kutokana na maswali mengi niliyoyapokea, nawapongeza wasomaji wetu kwa mapokeo ya somo lile lililosababisha niandike makala haya.

Ni ukweli usiopingika kuwa tatizo la kupoteza uwezo wa kuzaa linawaathiri kwa kiasi kikubwa wanawake kuliko wanaume.

Wanawake wengi ndiyo waathirika wakubwa kuliko wanaume inapofikia suala zima la afya ya uzazi na matatizo yake kwa ujumla.

Dalili kubwa inayoonyesha mwanamke hana uwezo wa kuzaa inaanzia pale anapopoteza uwezo wa kushika mimba baada ya kujaribu kwa kipindi cha miezi 6 na kuendelea.

Kupata hedhi inayozidi siku 35 na kuendelea na kupata pia hedhi iliyo chini ya mzunguko (chini ya siku 21), kuyumba kwa tarehe za hedhi au kutopata hedhi kwa baadhi ya miezi, kuna tafsiri kwamba mwanamke anakosa urutubishwaji wa mayai yake.

Wanawake wengi wamejikuta wanaangukia kwenye matatizo haya kutokana na sababu mbalimbali ambazo wakati mwingine zinachangiwa na aina ya maisha wanayoishi au hata matatizo ya kurithi na kupatwa na aina nyingine ya magonjwa ambayo yanaenda kuathiri mfumo wa uzazi moja mkwa moja.

Sababu zinazowafanya kutoshika mimba

Sababu ya kwanza ni matatizo katika urutubishwaji wa mayai. Matatizo katika urubishwaji wa mayai yanajitokeza baada ya mayai yanayokua hayajakomaa kwenye ovari zake au ovari zenyewe zinashindwa kuachia mayai yaliyokomaa hadi tarehe ambazo mwanamke zinamruhusu kushika mimba. Kitaalamu, tatizo hili linaitwa premature ovarian failure.

Tatizo hili huwa linawapata wanawake wengi na ni vigumu kwao kushika mimba.

Dalili za tatizo

Zipo dalili zinazoashiria kuwa mwanamke ana tatizo hilo ambazo ni pamoja na kukosa baadhi ya mizunguko yake ya hedhi.

Nyingine ni pale anapokaribia kupata hedhi, hujisikia maumivu ya kawaida ya tumbo au maumivu ya kawaida au muwasho kwenye matiti na maumivu ya kiuno.

Sababu nyingine ni baadhi ya matatizo yanayojitokeza kwenye mfuko wa uzazi.

Hata hivyo, wataalamu wa magonjwa ya wanawake wanasema wakati mwingine tatizo la kutopata ujauzito husababishwa na mwanamke mwenyewe.

Kwani baadhi yao wana tabia ya kutoa mimba kiholela bila kujua kuwa kufanya hivyo kunaweza kuwasababishia matatizo kwenye mfumo wa uzazi.

Kwani wengi wao hutoa mimba bila kufuata ushauri wa wataalamu wa afya.

Tatizo hilo linapaswa kufahamika kwa wanawake wenyewe kuwa utoaji wa mimba na hasa mara kwa mara bila kufuata ushauri wa wataalamu wa afya au madaktari husababisha kuacha baadhi ya mabaki ya uchafu wa mimba zilizoharibiwa kwenye mfuko wa uzazi bila wao kujua.

Hivyo, si ajabu kwa mwanamke huyu akashindwa kushika ujauzito hapo baadaye atakapoamua kuzaa, kutokana na mfuko wake wa uzazi kuvurugika.

Lakini pia baadhi ya matatizo mengine yanayojitokeza kwenye mfuko wa uzazi ni uwapo wa uvimbe ambao kitaalamu huitwa fibroids.

Na wakati mwingine nje ya ukuta wa mfuko wa uzazi kunaweza kujitokeza baadhi ya tishu zinazojijenga kwenye ukuta wa mfuko wa uzazi.

Tishu hizo zikikua na kuongezeka zinaweza kumletea mwanamke tatizo la kushindwa kubeba ujauzito.

Tatizo hilo kwa jina la kitaalaamu linaitwa endometriosis na ni muhimu kupata ushauri wa daktari ili kuchunguza uwezekano wa kuwapo kwa tatizo hilo.

Endometriosis mara zote huambatana na dalili za maumivu makali wakati wa hedhi au wakatiwa tendo la ndoa au kutokwa na damu nyingi wakati wa hedhi ikiambatana na mabonge mazito na maumivu kwenye mfumo wa uzazi hadi kwenye kiuno.

Ni vema kuwaona watoa huduma za afya ukiona dalili hizi mara moja.

Tatizo lingine ni mabadiliko yanayojitokeza kwenye mfumo wa homoni.

Wanawake wengi wanasumbuliwa na tatizo hilo bila kujijua. Kuyumba kwa uwiano wa mfumo wa homoni mwilini ni tatizo lingine ambalo kwa asilimia kubwa pia huwakumba wanawake.

Kisayansi, imethibitika kuwa kuyumba kwa mfumo wa homoni ni moja ya matatizo makubwa yanayowafanya wanawake washindwe kushika mimba.

Mchakato mzima wa upevushwaji na urutubishwaji wa mayai kwenye mfumo wa uzazi wa mwanamke kisayansi, unaratibiwa na mfumo wa homoni.

Hivyo, kuyumba kwa mfumo huo huathiri moja kwa moja mchakato mzima wa utungishwaji mimba.

Ni vema kumuona daktari kwa ajili ya vipimo kama ikitokea mwanamke anashindwa kupata ujauzito ili kubaini kinachosababisha tatizo hilo.

Sababu nilizozieleza ni chache kati ya nyingi zinazosababisha matatizo haya. Ushauri wangu ni kujenga ukaribu na watoa huduma za afya kwa ajili ya msaada wa uchunguzi na matibabu.