Nimonia ugonjwa unaokatisha maisha ya watoto wachanga

Muktasari:

  • Linasema takribani vifo 920,136 vilivyotokea mwaka 2015 kwa watoto, vinamechangiwa na nimonia.

Shirika la Afya Duniani (WHO) katika utafiti wake ilioufanya hivi karibuni, limebaini asilimia 16 ya vifo vya watoto chini ya miaka mitano vinasababishwa na nimonia.

Linasema takribani vifo 920,136 vilivyotokea mwaka 2015 kwa watoto, vinamechangiwa na nimonia.

Uchunguzi umeendelea kubaini kwamba moja kati ya vifo vitatu kwa watoto wachanga husababishwa na nimonia.

Mbali na hayo, nimonia ni moja ya maradhi 10 ya kwanza katika hospitali takribani zote nchini yanayowakumba watoto.

Chanzo cha maradhi hayo

Ugonjwa huu kwa asilimia kubwa husabishwa na bakteria, virusi pamoja na fangasi.

Bakteria aina ya Streptococcus pneumonia ameonekana kushika nafasi ya kwanza kwa kusabisha nimonia kwa watoto, akifuatiwa na Haemophilus influenzae type b (Hib).

Kwa upande wa virusi, kipo kinachojulikana kitaalamu kwa jina la respiratory syncytial virus.

Pia kuna fangasi aina ya Pneumocystis jiroveci wameonekana pia kuchangia robo ya vifo vya watoto wenye nimonia hasa wanaozaliwa wakiwa na maambukizi ya Virusi vya Ukimwi.

Pathofisiolojia Bakteria huweza kuingia kwenye mapafu kwa njia ya aspiresheni wanapofika kwenye mapafu.

Huko huvamia nafasi zilizo kati ya seli na kati ya alveoli, ambako makrofeji na nutrofili (seli nyeupe za damu zinazolinda) hujaribu kuwamaliza.

Nutrofili pia hutoa sitokini na kusababisha uamsho wa kijumla wa mfumo wa kingamwili.

Hii ndiyo inayosababisha mtoto kupata joto kali mwilini, kutetemeka na uchovu unaoshuhudiwa katika nimonia ya bakteria.

Nutrofili bakteria, na viowevu kutoka kwa mishipa ya damu iliyo karibu, hujaa katika alveoli na kusababisha konsolidesheni ionekanayo kwa eksirei ya kifua

Virusi vinafikaje kwenye mapafu

Virusi vinaweza kufika katika mapafu kwa njia mbali mbali ikiwamo ya kugusa kitu chenye virusi na kisha kushika pua. Maambukizi mengine ya virusi hutokana na matone kwenye hewa yaliyoambukizwa yakivutwa ndani hadi kwenye mapafu kupitia kinywani au puani.

Virusi vinapofika kwenye sehemu ya juu ya njia ya hewa, vinaweza kwenda hadi kwenye mapafu, huko huvamia seli zilizoko kwenye kuta za njia za hewa, alveoli au parenkaima za mapafu.

Virusi vingine kama vya ukambi na hepesi simpleksi, vinaweza kufika kwenye mapafu kupitia kwenye damu. Uvamizi wa virusi hivi kwenye mapafu unaweza kusababisha viwango tofauti vya vifo vya seli.

Kwani mfumo wa kingamwili ukijaribu kuitika kwa maambukizi haya, uharibifu zaidi wa mapafu unaweza kutokea.

Seli nyeupe za damu, hasa za mononuklea, kwa kawaida husababisha athari hiyo. Pamoja na kuharibu mapafu, virusi vingi huathiri ogani zingine wakati huohuo na kukatiza shughuli zingine za mwili. Virusi pia huufanya mwili kuwa mwepesi wa kuathiriwa na maambukizi ya bakteria; kwa njia hii, nimonia ya bakteria inaweza kutokea kama ugonjwa ambatani.

Namna ya kuitambua nimonia.

Shirika La Afya Duniani WHO limefafanua kiafya kuhusu nimonia ya watoto kwa msingi wa kikohozi au upumuaji mgumu na kiwango cha haraka cha kupumua, kujivuta ndani kwa kifua, au kiwango kilichopungua cha fahamu.

Kiwango cha haraka cha kupumua hufafanuliwa kama zaidi ya pumzi 60 kwa kila dakika kwa watoto chini ya umri wa miezi 2, pumzi 50 kwa dakika kwa watoto wa umri wa miezi 2 hadi mwaka 1, au zaidi ya pumzi 40 kwa dakika kwa watoto wa umri wa mwaka 1 hadi miaka 5. Kwa watoto, kiwango kilichoongezeka cha kupumua na kujivuta ndani kwa sehemu ya chini ya kifua ni vyepesi kuhisi kuliko kusikiliza milio ya kifua kwa stethoskopu.

Namna ya kuzuia nimonia

Uchanjaji huzuia nimonia za baadhi ya bakteria na za virusi kwa watoto na hata watu wazima.

Chanjo ya influenza ni bora dhidi ya influenza A na B.

Juhudi zinazofanywa na Taasisi ya Udhibiti na Uzuiaji wa Maradhi, imependekeza uchanjaji wa kila mwaka kwa kila mtu aliye na umri wa miezi sita na zaidi.

Kuwapatia wahudumu wa afya kingamaradhi, hupunguza hatari ya nimonia ya virusi miongoni mwa wagonjwa wao. Chanjo dhidi ya streptokokasi nimonia na haemofilasi influenza, nazo zinaendelea kutolewa.

Kuwapatia watoto chanjo dhidi ya streptokokasi numoniae kumepelekea kupungua kwa visa vya maambukizi haya kwa watu wazima kwa sababu wengi wao hupata maambukizi kutoka kwa watoto. Chanjo zingine zinazokinga nimonia ni kifaduro, tetekuwanga na ukambi.

Mambo mengine ya kuzingatia ni kama vile kutibu maradhi fiche (yakiwamo ya VVU/Ukimwi na utapiamlo) ipasavyo, kunaweza kupunguza hatari ya nimonia.

Namna ya kuwakinga watoto wachanga

Kwa watoto wa chini ya miezi sita, inashauliwa kuwanyonyesha bila kuwapa chakula kingine ili kupunguza hatari na ukali wa ugonjwa.

Wajawazito inapendekezwa wachunguzwe Streptokokasi ya kundi B na Klamidia trakomatisi na kutoa matibabu kwa antibiotiki ikihitajika.

Hii husaidia kupunguza viwango vya nimonia kwa watoto wachanga.

Mbinu za kuzuia maambukizi ya VVU kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto huenda ikafaa pia.

Dk Kammu keneth, 0759 775788 Katika jitihada za kuokoa maisha ya mama na mtoto.