Njia rahisi ya kuboresha maisha ya mtoto mwenye maambukizi ya VVU

Muktasari:

  • Zipo njia rahisi ambazo mzazi au mlezi anapaswa kuzifuata ili kumuweza kuishi na mtoto mwenye VVU na kumsaidia kuboresha maisha yake ikiwamo kuishi maisha marefu na kufikia malengo yake.

Kuishi na mtoto mwenye maambukizi ya Virusi vya ukimwi ni jambo linalohitaji umakini ili kumeupusha na madhara ya maambukizi haya pamoja na maradhi nyemelezi.

Zipo njia rahisi ambazo mzazi au mlezi anapaswa kuzifuata ili kumuweza kuishi na mtoto mwenye VVU na kumsaidia kuboresha maisha yake ikiwamo kuishi maisha marefu na kufikia malengo yake.

Yafuatayo ni mambo ambayo kama yakifanyika yana tija kwa afya ya mtoto mwenye VVU, kwani humsaidia kuepukana na matatizo mbalimbali ya kiafya yatokanayo na maradhi sugu na nyemelezi.

Zingatia ushauri na matibabu

Mzazi au mlezi anapaswa kupata ushauri nasaha toka kwa wataalamu wa afya wenye mafunzo maalumu ya VVU na Ukimwi.

Hili ni jambo muhimu kwani itamfanya alifahamu tatizo na namna yakukabiliana nalo.

Mzazi au mlezi akipata elimu hiyo, ndiyo itamsaidia kuitumia kulinda afya ya mtoto mwenye maambukizi.

Kama mtoto mwenye VVU alishaanza matibabu ya dawa za kufubaza makali ya VVU na dawa za kuzuia maradhi nyemelezi, hakikisha mtoto anapata dawa bila kukosa.

Ikumbukwe, dawa hizi anapaswa kuzitumia katika maisha yake yote na ndizo zinazomwongezea muda wa kuishi na kadri anavyotumia ARV, ndivyo kinga ya mwili na afya yake huimarika.

Ushauri nasaha

Ushauri nasaha na kufahamu umuhimu wa dawa za ARV, inamsaidia mlezi au mzazi kufuatilia matibabu ya mtoto na kumjengea imani na dawa hizo tangu akiwa mtoto.

Kumjenga kitabia

Kumjenga kitabia mapema kuna faida kubwa kwani humfanya asiache kutumia dawa hata akiwa mkubwa.

Kwani akizoea kutumia dawa hizo, kutamfanya aishi maisha marefu.

Na hata inapobaini anaugua maradhi mengine, inakuwa rahisi kumuwahisha hospitali kupata huduma.

Kumbuka kinga ni bora kuliko tiba.

Watoto wenye VVU wapo katika hatari zaidi ya kushambuliwa na maradhi ukilinganisha na wengine.

Mlo kamili

Mlo kamili huwa na vyakula mchanganyiko yaani wanga, protini, mafuta, mboga za majani, matunda na unywaji wa maji yakutosha.

Vyakula hivi ndivyo vinavyotupa nguvu na joto pia kujenga mwili na kinga ya mwili.

Mlo kamili haimanishi ni mlo wenye gharama kubwa, jamii yetu imezungukwa na vyakula vyakiasili vinavyopatikana kirahisi. Mfano mboga za majani kama mchicha, matembele na karoti. Pia vyakula vya protini yakiwamo maharagwe ya soya, kunde, njegere na matunda ni maembe, machungwa na matikiti maji.

Matunda na mboga mboga zimesheheni virutubisho na madini mbalimbali yanayosaidia kujenga kinga ya mwili.

Hivyo ni jambo la msingi mzazi au mlezi kulima bustani za mboga na matunda na si vibaya kufuga kuku wakienyeji kwa ajili ya mayai na nyama (chanzo cha protini).

Mboga mboga, matunda, na protini ni muhimu sana katika ujenzi wa kinga ya mwili.

Ikumbukwe mtoto mwenye VVU ni rahisi kushambuliwa na maradhi kwa sababu kinga yake inakua dhaifu na bado ni mdogo.

Mtoto mwenye VVU ambaye tayari ni mkubwa, anahitaji kupata mapumziko yakutosha zaidi ya saa 8 kila siku, hii husaidia kinga ya mwili kuimarika.

Faida ya Michezo

Kwa watoto wenye umri wa miaka 2 na kuendelea, michezo ya kitoto na wenzake humfanya awe na mwili imara na mwenye furaha.

Furaha humpatia hisia chanya hivyo kumuepusha na matatizo ya kiakili.

Mpe mahitaji mbalimbali ikiwamo kumnunulia vifaa vya kuchezea kama mipira na midoli.

Kumjenga kisaikolojia

Ikianzia kwa mzazi kukubaliana na hali halisi baada ya kuelewa ushauri aliopewa ni jukumu lake kumjenga kiakili mtoto wake.

Mzazi au mlezi anapaswa kumkuza mtoto vizuri kwa kumuonyesha upendo na furaha.

Mfanye mtoto huyo asijione yuko tofauti, pale atakapofikia umri wa kuanza kutambua, ni vizuri akawa anaelimishwa mambo mbalimbali yenye tija na afya kwake.

Hapo baadaye ataweza kuelimika na kukubaliana na hali yake bila kupatwa na msongo wa mawazo au sonona.

Kwani uwapo wa mambo haya mawili huweza kumfanya asiwe na afya njema.

Haki ya kupata malezi bora

Watoto wenye VVU nao wanahitaji malezi bora kuanzia kwa wazazi au walezi mwishowe na jamii kiujumla.

Watoto hawa wanahitaji kulelewa kwa kuelekezwa na kufundishwa mambo mema.

Lengo la kufanya hayo ni kuwajenga kitabia na kupata hisia nzuri, kuzungumza nao na kuwaelekeza pasipo adhabu ni jambo la msingi.

Ni kawaida kwa watoto hawa kukasirika kirahisi na kupoteza hisia nzuri.

Ni vizuri kufahamu watoto hawa wana udhaifu mkubwa ukilinganisha na watoto wengine. Mfano ni rahisi kupata huzuni haraka, huwa na hasira na wakali.

Haki ya kupata elimu

Haki ya kupata elimu kwa watoto hawa huwa ni ya lazima kama watoto wengine, na itakapofikia muda wa kuanza shule ni vizuri nao wakapelekwa, tayari kuna sheria zinazowalinda watoto hawa kwa baadhi ya nchi.

Mtengenezee mazingira bora ya kuishi

Pale unapokuwa umemwekea mazingira bora ya ndani na nje ya nyumba, humfanya ajihisi mwenye utulivu wa kimwili na kiakili.

Weka mazingira safi ya mahali anapolala, anapotumia kwa ajili ya kupata chakula na anapocheza.

Hakikisha mtoto anakuwa msafi kimwili na nguo anazovaa. Hali hii itamfanya kuvutiwa na mazingira hayo na kuyapenda.

Uwazi wa tatizo

Ni vizuri kuweka wazi tatizo la mtoto wako kwa watu wa karibu katika hatua za awali na baadaye si vibaya kuwaeleza wanajamii muhimu kama viongozi wa mitaa na vijiji na shuleni kwa walimu wake, ingawa jambo hili huwawia vigumu.

Wengi huhisi wanaweza kutengwa na kunyanyapaliwa, lakini kutokana na elimu ya afya kuendelea kusambaa kwa kiasi fulani, jamii imeanza kuelewa na kuacha unyanyapaa na kuwatenga.

Ingawa bado inakubalika suala la kuweka wazi linabaki kuwa kwa mtoto, wazazi na walezi.

Ni muhimu kupata ushauri nasaha kuhusiana na jambo hili la kuweka wazi juu ya hali ya mtoto.

Kushirikiana na makundi muhimu

Kujenga uhusiano mwema na makundi kama ya wahudumu wa afya, kunasaidia kupata msaaada wa haraka na taarifa mpya, hivyo kujiongezea elimu ya afya ya namna ya kuishi na mtoto wako.

Kujenga urafiki mzuri na familia zingine ambazo nazo zimepata tatizo kama hilo, inasaidia kubadilishana mawazo, matumaini na faraja kwani hiyo ni moja ya nyenzo muhimu ya kupambana na unyanyapaa unaofanya na baadhi ya wanajamii wasio na uelewa na tatizo hili.

Ukaribu na watu kama walimu, maofisa ustawi wa jamii, washauri nasaa.

Hawa ni watu muhimu kwa malezi na husaidia kumjenga mtoto wako kisaikolojia.

Ikimbukwe mwalimu ndiye mlezi wake pale anapokuwa shuleni na ofisa ustawi wa jamii ni kiungo muhimu kati ya mtoto na jamii inayomzunguka.

Makundi mengine ni viongozi wa serikali za mitaani na viongozi wa dini, viongozi wa mtaa husaidia pia kuwaelewesha wanajamii tatizo mlilonalo na pia huwa na msada wa kupambana na unyanyapaa na kutengwa na jamii.

Kwakuwa jamii yetu huwa na imani zetu si vibaya kumjenga kiimani mtoto uliye naye ili aishi kwa matumaini.

Viongozi wa dini tayari wengi wana uelewa na wamepewa elimu juu ya mambo ya Ukimwi na wana msaada mkubwa katika maisha ya kila siku ya watu wanaoishi na virusi vya ukimwi na wale wanaougua Ukimwi.