PIRAMIDI YA AFYA: Wasiotahiriwa wako hatarini

Hivi karibuni tuliona umuhimu wa tohara kwa wanaume, leo nitazumgumzia saratani ya sehemu za siri za mwanaume.

Pale tishu za sehemu hizo  zinapovamiwa na seli zenye saratani zinazoweza kukua bila mpangilio, ndipo hujitokeza.

Muathirika humchukua miaka miwili kupoteza maisha kama hatua za tiba hazitachukuliwa.

Maambukizi ya virusi vya Papilloma kwa mwanaume asiyetahiriwa humweka zaidi kwenye hatari ya kupata saratani hiyo.

Saratani ya sehemu za siri ya mwanaume huwatokea mara chache ukilinganisha na saratani ya tezi dume inayoongoza kuwapata wanaume wengi na huwasababishia vifo.

Wanaume wenye umri mkubwa wasio wasafi wa mwili ndiyo wanapatwa zaidi na saratani hii.

Saratani yoyote inapompata mwanadamu na ikapiga hatua za mbeleni huwezi kuwa na madhara makubwa ikiwamo kusambaa katika maeneo mbalimbali mwilini na kusababisha vifo.

Vihatarishi vya kupata saratani hiyo ni pamoja na kutofanyiwa tohara, maambukizi ya virusi vya papiloma ambayo huwapata zaidi wasiotahiriwa, kujamiana bila kinga na kuwa na wapenzi wengi.

Mambo mengine ni pamoja na utumiaji wa tumbaku, watu wenye zaidi ya miaka 60, kuwa na tatizo la kuzaliwa na ngozi ya mbele (govi) kushindwa kurudi nyuma (kufeduka), kitabibu hujulikana phimosis, kutokuwa msafi wa mwili na kuugua magonjwa ya zinaa.

Haimaanishi kuwa mwanaume akiwa na vihatarishi hivyo ndiyo lazima apate saratani hiyo, na pia, haimaanishi kuwa asiye na vihatarishi hivyo hawezi kuugua saratani hiyo.

Dalili na viashiria ni pamoja na kuwashwa au kukereketwa eneo la uume, tishu eneo la uume kuwa jekundu, kuwa na uvimbe, uwapo wa kakidonda katika uume, kutoa uchafu kama majimaji na kuvuja damu katika eneo lenye kidonda.

Pale saratani inaposambaa maeneo jirani ikiwamo kiunoni na eneo la njia ya haja kubwa na yale ya mbali kama ini na mapafu, dalili itategemea na mahali ilipovamia.

Dalili za baadaye katika hatua za mwishoni za ugonjwa huo ni pamoja na uzito wa mwili kupungua, kukonda sana, kupungukiwa na damu, kuchanganyikiwa na kupata sonona (depression).

Matibabu ya saratani hiyo hutegemea na hatua iliyofikia. Hivyo, hapa ndipo hatua ya kunyofoa sampuli ya tishu kwa ajili ya uchunguzi wakimaabara ili kujua hatua ya saratani ilipofikia.

Inapobainika iko katika hatua za awali, huweza kutibika kwa upasuaji kwa kuondoa sehemu ya ngozi au sehemu ya uume.

Katika hatua za mbeleni yaani hatua ya tatu kuendelea, matibabu huwa ni kwa tiba ya mionzi na dawa za kemikalitiba.

Endapo itabainika imeisha sambaa maeneo mbalimbali mwilini na ni vigumu kutibika, mgonjwa hupewa matibabu maalumu kwa ajili ya kumpunguzia maumivu, kumwongezea damu na lishe maalumu. Hapo ndipo mgonjwa hupatiwa pia ushauri maalumu kwa ajili ya kumwezesha kukubaliana na hali hiyo. Ndugu pia hupatiwa elimu ya namna ya kuishi na mgonjwa wao kwa lengo la kumsaidia na kumpatia faraja.

Nihitimishe kwa kuwashauri wale wote ambao hawajafanyiwa tohara, kufika katika huduma za afya kwa ajili ya kufanyiwa tohara.

Wajitokeze pia katika kliniki maalumu za madaktari wanaotembelea mikoani ambao huwafanyiwa tohara bure. Hakikisha unaepuka vihatarishi nilivyoorodhesha hapo juu.

Fika katika huduma za afya mapema pale unapoona dalili.

0763-296752