Pamoja programu yaja na mbadala wa kulinda kinywa

Muktasari:

  • Hivyo, ni vyema kujua kama mtu unatatizo la kiafya, unapaswa kwenda kuwaona wataalamu wa afya kwa ushauri zaidi.

Ni kawaida kusikia uvumi miongoni mwa watu ambao si wataalamu wa afya wakiueneza kwa juhudi kubwa bila kujua au kujua wanapotosha umma.

Hivyo, ni vyema kujua kama mtu unatatizo la kiafya, unapaswa kwenda kuwaona wataalamu wa afya kwa ushauri zaidi.

Wapo watu wengi ambao hawafahamu ukweli juu ya umuhimu wa kutunza kinywa, na mara wapatapo maambukizi ya maradhi ya kinywa, hawafiki hospitali kwa ajili ya kupata tiba.

Kijana Ibrahimu Juma alisafiri kwenda kijijini kwao kwa ajili ya likizo, bahati mbaya aliugua jino, akamweleza bibi yake kuhusiana na hali hiyo.

Lakini badala ya bibi kumweleza mjukuu wake huyo aende hospitali akatibiwe, alikimbilia kwa jirani yake kuomba msaada wa tiba.

Kwa mujibu wa Ibrahimu, bibi alimletea kipande cha mavi ya ng’ombe yaliyokauka akamtaka akate kidogo na abandike kwenye jino linalomuuma, akidai ni tiba sahihi jambo ambalo si sahihi.

Huo ni mfano mmoja tu wa imani potofu iliyojengeka miongoni mwa watu kuhusiana na tiba sahihi ya kinywa ni ipi.

Lakini wapo watu hudai kupiga mswaki mara nyingi na kwa nguvu huzuia kuoza kwa meno.

Wataalamu wa tiba ya kinywa wanaonya kuwa kupiga mswaki mara nyingi na kwa kutumia nguvu, kunaweza kusababisha kukwangua sehemu ngumu ya nje ya jino, kulifanya laini na hatimaye kuuma au hata kuvunjika.

Kupiga mswaki mara mbili, taratibu na kwa njia sahihi ndicho kinachosaidia meno kuwa na afya

Wengine husema mtu hana haja ya kumuona daktari wa meno kama hajaugua.

Lakini kwa mujibu wa madaktari wa meno, kila mtu anatakiwa kuchunguzwa kinywa mara kwa mara.

Kwani siyo meno yote yanayoonekana mazuri na imara ni mazima, mengine yanaweza kuwa yameharibika hasa yale ambayo yako sehemu za ndani ambazo si rahisi kuonekana.

Hata hivyo, baada ya kubaini changamoto nyingi zinazowakabili wananchi kuhusiana na tiba ya kinywa, hivi karibuni Chama cha Madaktari Wanafunzi wa Afya ya Kinywa Tanzania (Tanzania Dental Students Association-TDSA) wakishirikiana na Chama cha madaktari wanafunzi wa afya ya kinywa wa nchi za Ulaya (European Dental Students Association –EDSA) na Chuo kikuu cha afya na sayansi shirikishi Muhimbili (MUHAS) waliungana kutoa huduma za uchunguzi wa kinywa na matibabu kwa wanafunzi wa Shule za msingi za Uhuru Mchanganyiko, Buguruni na Shule ya Nyamata Academy, zote za Jijini Dar es Salaam.

Madaktari hawa wameanzisha program maalumu iitwayo ‘Pamoja’ ikilenga kutoa elimu na kutibu maradhi ya kinywa kwa wanafunzi.

Rais wa TDSA, Evarist Mulyahela anasema hii ni awamu ya tatu kufanyika tangu ilipoanzishwa mwaka 2015.

“Awamu hii ya tatu tuliianza Septemba 9 na tukaihitimisha Septemba 22, tuliwahudumia wanafunzi wa Shule ya Msingi Uhuru Mchanganyiko ambayo ina wanafunzi walemavu pia, hivyo kufanya kuwa ya kipekee tukilinganisha na awamu mbili zilizopita za 2015 na 2016,” anasema Mulyahela na kuongeza: “Huduma hii tuliitolea Chuo Kikuu cha Afya Muhimbili.”

Anasema zaidi ya wanafunzi 1,000 walipatiwa elimu ya afya ya kinywa kwa vitendo, namna sahihi ya kupiga mswaki kwa ufanisi.

Mulyahela anasema wanafunzi 838 walifanyiwa uchunguzi wa kinywa bure na kati yao asilimia 51 wasichana na asilimia 1.6 walemavu.

Wanafunzi 297 walipatiwa aina tofauti ya matibabu ya maradhi ya kinywa yaliyobainika.

“Matibabu tuliyoyatoa ni pamoja na kuziba meno, kusafisha na kung’oa yaliyobainika kuharika kwa kiwango kikubwa.

Licha ya kutoa huduma hiyo kwa wanafunzi, madakatri hao walitoa pia elimu kwa walimu wa shule hizo ili kurithisha elimu hiyo ya afya ya kinywa, ambayo pia wataweza kuwafundisha wanafunzi mara kwa mara kwenye vipindi vyao darasani.

Changamoto ya matibabu ya kinywa

Ofisa Programu wa Pamoja, Protus Musungu anasema bado kuna changamoto nyingi za kukabiliana na maradhi ya kinywa zinazowakumba madaktari na wataalamu wa afya ya kinywa.

Anataja changamoto mojwapo ni ukosefu wa vifaatiba kwenye maeneo wanayofika kutoa huduma.

Musungu anasema kulingana na muundo wa program wanayoifanya, wanauhaba wa viti vya matibabu vinavyohamishika pamoja na vifaatiba vya meno.

“Lakini pia tatizo la wakarimani kwa wanafunzi wenye ulemavu wa kusikia pia lilitupatia shida,” anasema Msungu.

Hata hivyo, anasema ili elimu ya kulinda afya ya kinywa iweze kufika kwa Watanzania wote, kuna haja kwa wadau mbalimbali wa afya nchini, kushirikiana na Serikali kuhamasisha kufanyika kwa uchunguzi wa afya ya kinywa kama yalivyo maradhi mengine kwa wananchi. Tunakaribisha wadau mbalimbali kuchangia “Pamoja kama tutasaidiwa upatikanaji wa vifaatiba vitakavyotuwezesha kuifanya kazi hii, tuko tayari muda wowote,” anasema ofisa huyo.

Msungu anasema umefika wakati wa kuongeza nguvu ya kuihamasisha jamii ijenge utamaduni wa kwenda hospitali kwa uchunguzi wa afya ikiwamo afya ya kinywa angalau mara moja kwa mwaka.

Anasema hiyo itasasidia kugundulika mapema kwa matatizo yoyote ya kiafya na kuwezesha utatuzi wa mapema kufanyika.

Wakati Msungu akitoa ushauri huo kwa jamii, wataalamu wa kinywa na meno wao pia wanaianisha namna ya kutunza meno ya watoto.

Dk Onesmo Sayo anasema wazazi wanapaswa kuanza kusafisha kinywa cha mtoto siku chache baada ya kuzaliwa kwa kufuta fizi zake kwa kitambaa safi kibichi.

Anasema mara tu meno yaanzapo kuonekana, hapohapo huweza kuanza kutoboka.

Dk Shayo anasema meno ya mbele ya utotoni huweza kujitokeza kinywani miezi sita baada ya kuzaliwa, ingawa baadhi ya watoto huweza kuchelewa kuota meno hadi anapofikisha miezi 12 au 14.

Hata hivyo, anasema ni vyema mzazi akajiridhisha mtoto wake anaweza kupiga mswaki mwenyewe kinyume cha hapo anashauri mzazi au mlezi aendelee kumpigisha mswaki mara mbili kwa siku kwa kutumia mswaki wa kitoto pamoja na dawa ya meno yenye madini ya floridi kiasi cha ukubwa wa punje ya maharage.

“Wakati mtoto anapokuwa na meno mawili yanayogusana tayari, anza kumzoesha kuflosi kila siku,” anasema daktari huyo.

Watoto Wa Umri Chini ya Miaka Mitatu

Kwa watoto wenye umri wa chini ya miaka 3, wazazi ama walezi lazima waanze kumpigisha mswaki mara tu meno yanapoanza kutokeza kinywani, mswaki huo uwe ni mdogo na dawa ya meno yenye madini ya floridi kidogo kiasi cha ukubwa wa punje ya mchele.

Ni lazima kupiga mswaki kwa umakini asubuhi baada ya kifungua kinywa na usiku kabla ya kulala. “Hakikisha mtoto hamezi dawa ya meno aliyotumia kupigia mswaki, badala yake ateme yote na kusukutua na maji,” anashauri.