Sio kila uvimbe kwenye mfuko wa uzazi ni saratani

Muktasari:

Dhana hii imezua hofu kubwa kwa miongoni mwa wanawake wengi hasa inapotokea vipimo vikagundulika wana uvimbe ulioota kwenye mifuko yao uzazi.

Moja ya dalili za saratani za aina nyingi huambata na uwapo wa uvimbe wa aina mbalimbali kwenye sehemu husika ya mwili kulingana na aina ya saratani.

Dhana hii imezua hofu kubwa kwa miongoni mwa wanawake wengi hasa inapotokea vipimo vikagundulika wana uvimbe ulioota kwenye mifuko yao uzazi.

Habari njema ni kwamba, uvimbe huo hautokani na ugonjwa wa saratani, bali husababishwa na sababu nyinginezo kama nitakavyoeleza, ila kwa kuwa hautokani na saratani, sio vyema kufumbia macho kwa sababu zina madhara mengine kwenye mfumo wa uzazi na afya.

Uvimbe huo huitwa uterine fibroids kwa kitaalamu,ni uvimbe usiotokana na saratani na mara zote huwa unaota na kukua kwenye ukuta au tabaka lililopo kwenye mfuko wa uzazi.

Uvimbe huu hutofautiana kwa ukubwa wa maumbile na wakati mwingine ukicheleweshwa unaweza kufikia hata ukubwa wa tikiti maji.

Pia, hutofautiana kwa idadi kati ya mwanamke mmoja na mwingine, mwanamke mmoja anaweza akaotwa na uvimbe zaidi ya mmoja kwenye mfuko wake wa uzazi, lakini mwanamke mwingine anaweza akaotwa na uvimbe mmoja tu kwenye mfuko wake na mara nyingi moja ya madhara yanayosababisha na uvumbe huo ni mkandamizo wa mfuko wa uzazi, huulazimisha kupanuka hadi kugusa kwenye viwambo vya mbavu na hapo ndipo matatizo mengine hujitokeza.

Hata hivyo, wanawake wengi hupatwa na tatizo hilo kwenye mifuko yao uzazi, lakini wengi wao hawatambui kama wanalo kwa sababu hauonyeshi dalili hadi unapokuwa mkubwa kupita kiasi na kuanza kuleta matatizo kiafya.

Nawashauri wanawake ni vyema wakajenga utamaduni wa kupata vipimo mara kwa mara ili kubaini ukiwa katika hatua za awali na kwa kufanya hivyo, watajiepusha na madhara makubwa ya kiafya yasababishwayo na uvime huo.

Kama nilivyoeleza hapo juu, uvimbe huchukua muda hadi kuanza kuonyesha dalili zake, kama mwanamke mwenyewe hana utamaduni wa kupata vipimo mara kwa mara; au kama utakuwa umedumu kwa muda mrefu, anaweza kuziona dalili kama vile za hedhi iliyopitiliza ambayo baadaye inaweza kumsababishia kupata anemia, maumivu ya mgongo na kiuno. Pia anaweza kupata haja kubwa kwa shida, maumivu makali chini ya kitovu na hasa ikitokea uvimbe umeshakuwa mkubwa, kupata haja ndogo mara kwa mara kuliko kawaida na kupata maumivu makali wakati wa tendo la ndoa.

Ukiona dalili hizi, ni dhahiri una tatizo hilo na ni vyema kwenda hospitali kwa ajili ya vipimo na mpango wa matibabu. Uvimbe unaoota kwenye mfuko wa uzazi japo hauwezi kusababisha saratani, lakini una madhara mengine makubwa kiafya ambayo ni pamoja na matatizo wakati wa kujifungua yanayoweza kuhatarisha maisha ya mama na mtoto hasa kama atakuwa alishika ujauzito akiwa tayari ana uvimbe. Lakini pia uvimbe huweza kusababisha mwanamke kukosa uwezo wa kushika mimba, mimba kutungwa nje ya uzazi na tatizo lingine kubwa ni mimba kuharibika mara kwa mara. Sababu kubwa zinazochangia tatizo hili ni mtatizo yanayojitokeza kwenye mfumo wa homoni.

Kisayansi, kwenye mwili wa mwanamke kuna homoni (vichocheo) za estrogen na progesterone, huwa zinafanya kazi ya kuchochea maendeleo ya ukuaji wa sehemu ya ndani ya mfuko wa uzazi kwenye kila mzunguko wa hedhi wa kila mwezi.

kwa ajili ya maandalizi ya urutubishwaji wa mayai na utungishwaji wa mimba, sasa wakati mwingine huwa inatokea homoni hizi hujichochea zaidi ya kiwango na hivyo kuanza kutengeneza vimbe ndogo ndogo kwenye ukuta wa mfuko wa uzazi.

Lakini pia tatizo hili linahusishwa sana na sababu za kurithi. Ni vyema kwa mwanamke kuijua vizuri historia ya ukoo wake ili kutambua kama naye yupo kwenye hatari ya kurithi ugonjwa huu au la! Kwa sababu mara nyingi pia mtu anaweza kuupata ugonjwa huu kupitia vinasaba kutoka kwa watangulizi wake kwenye ukoo.

Sababu zingine zinazocchangia kwa kiasi kikubwa sana tatizo hili ni pamoja na kupata hedhi katika umri mdogo zaidi, matumizi ya baadhi ya njia za uzazi wa mpango, uzito wa mwili kupitiliza, ukosefu wa vitamin D, na hata ulevi pia.