Tambua namna uso unavyoweza kuainisha ubora wa afya yako

Muktasari:

Na kwa kupitia maumivu hayo, ndipo tunaanza kutambua kuwa afya zetu haziko sawa na huenda kuna baadhi ya maradhi ynaashiria kutushambulia, hivyo ni lazima kuchukua hatua ya kupata matibabu haraka kabla hali haijawa mbaya.

Uchovu, maumivu ya viungo sambamba na ya mwili mzima au maumivu ya tumbo na kichwa, ni baadhi tu ya dalili ambazo wengi tumezizoea.

Na kwa kupitia maumivu hayo, ndipo tunaanza kutambua kuwa afya zetu haziko sawa na huenda kuna baadhi ya maradhi ynaashiria kutushambulia, hivyo ni lazima kuchukua hatua ya kupata matibabu haraka kabla hali haijawa mbaya.

Lakini kila tunapojiangalia kwenye vioo, nyuso zetu pia zinasema mengi kuhusu afya zetu.

Baadhi ya maradhi mengi yanayoweza kuleta madhara makubwa kiafya yanaweza kutambuliwa kwa dalili zinazojitekeza kwenye uso wa binadamu.

Kujiangalia kwenye kioo ni jambo la kawaida ambalo twatu hulifanya karibu kila siku.

Lakini mtu anapojiangalia kwa makini, wakati mwingine anaweza kuyaona mabadiliko madogo yanayojitokeza usoni.

Mabadiliko haya yanaweza kudhani niwa ni ya kawaida, lakini ukweli ni kwamba hayapaswi kufumbiwa macho kwa sababu yanaashiria matatizo fulani ya kiafya.

Kwa mfano rangi ya ngozi na jicho kubadilika na kuwa ya njano.

Hii ni homa ya manjano. Inatokea pale mtu anapokuwa na uchafu mwingi mwilini au takamwili.

Hali hii huwa ni ya kawaida na isiyokuwa na madhara kwa watoto wachanga wenye umri wa wiki 38 hadi 40 kwa sababu maini yao bado hayajakomaa kama yanavyotakiwa.

Lakini kwa watu wazima, homa ya manjano inaweza kuashiria matatizo makubwa zaidi ya kiafya kama ya maambukizi ya aina mbalimbali ya virusi vinavyoshambulia ini (hepatitis) na maradhi ya ini ua matatizo ya kongosho au madhara yatokanayo na utumiaji wa vilevi.

Chunusi sugu:

Mara chache unaweza kupata chunusi au vipele vyeusi usoni. Hivi mara nyingi vinaashiria aleji ya chakula au matumizi ya baadhi ya sabuni za kuogea na mchafuko wa damu na baada ya muda hutoweka.

Lakini ni vema kufanya vipimo inapotokea chunusi hizo zinakuwa sugu. Kwa kufanya hivyo, kutasaidia kutambua dalili za maradhi mengine mapema hasa ya saratani ya ngozi.

Vidonda vinavyojitokeza pembeni ya mdomo mara nyingi vinasababishwa na baridi au na maambukizi ya ugonjwa wa zinaa unaotokana na kufanya ngono kwa njia ya mdomo au tabia ya kunyonya via vya uzazi wakati wa tendo la ndoa.

Maambukizi yanayopatikana kupitia njia hii yanasababishwa na aina fulani ya virusi kitaalamu vinaitwa herpes viruses.

Unapopata maambukizi ya virusi hivyo, vinabaki kwako na baada ya muda vinatengeneza vidonda na malengelenge mdomoni.

Wakati mwingine pia ni kawaida kutokwa na vidonda vidogo nje ya mdomo baada ya maumivu makali ya kichwa, uchovu kupita kiasi, homa, sababu za kisaikolojia na hasa kuwa na wasiwasi, na kupigwa na jua kwa muda mrefu.

Vidonda vinavyotokana na sababu kama hizo hutoweka vyenyewe baada ya muda, lakini kama vinajitokeza mara kwa mara na vinadumu kwa muda mrefu,ni vema kumuona daktari ili kupata tiba.

Mipasuko mdomoni:

Kila mmoja anapitia hali hiyo ya lipsi za mdomo kukauka na kutoa mipasuko midogo midogo kwa kipindi tofauti.

Mara nyingi husababishwa na hali ya hewa na hasa ya baridi, au kushuka kwa mfumo wa kinga mwilini kwa kipindi husika.

Tatizo hilo mara nyingi hudumu kwa muda mfupi na kutoweka. Lakini pia ni vema kutumia vilainishi vya kupaka mdomoni ili kuzuia lisiendelee.

Vilainishi vinapatikana kwenye maduka ya dawa na hata kwenye maduka ya vipodozi.

Japo tatizo hili hutoweka baada ya muda, lakini ni vema mtu akawa makini linapotokea mara kwa mara.

Kubabuka ngozi ya uso

Wakati mwingine kubabuka kwa sehemu ndogo ya uso hakuwezi kuleta tatizo kiafya na mara nyingi hutoweka baada ya muda.

Lakini mtu anapaswa kuwa makini anapoona hali hiyo imeenea sehemu kubwa ya uso. Tatizo hilo huwa si lakawaida. Kitaalamu linaitwa butterfly rash. Linapotokea usoni, ngozi hubabuka na sehemu iliyoathirika hutengeneza muonekano wa kipepeo.

Mara zote hiyo huwa ni ishara yakushambuliwa na ugonjwa unaoitwa “lupus”.

Huo ni ugonjwa unaotokea wakati mfumo wa kinga za mwili, badala ya kuulinda mwili dhidi ya maradhi nyemelezi, unageuka na kushambulia tishu na ogani za mwili.

Pamoja kupata ishara hiyo usoni, ugonjwa huo pia huambatana na ishara zingine kama za homa kali, sehemu za maungio kuhisi kukauka na kukaza, uchovu uliokithiri na joto la mwili kupanda kuliko kawaida.

Ukibaini hali hiyo, muone daktari haraka.

Kuota nywele sehemu ambazo sio za kwaida

Hali hiyo mara nyingi huwatokea wanaume kadiri wanavyozidi kukua na hasa sehemu za kuzunguka masikio na sehemu zinazokaribiana na macho. Na wananwake wao huota ndevu .

Wanawake wenye chini ya miaka 30 wanaoota nywele sehemu za usoni na hasa kidevuni, inaweza ikawa ni ishara ya ugonjwa unaoshambulia ovari na kitaalamu unaitwa polycystic ovary syndrome.

Tatizo hilo linaweza kumfanya mwanamke apoteze uwezo wa kushika mimba na kuzaa.

Madoa ya rangi ya pinki usoni

Tatizo hili linaitwa melasma. Ugonjwa wa ngozi ya uso ambao unasababisha madoa yenye rangi ya pinki kwenye ngoi ya uso.

Mara nyingi unasababishwa na ujauzito, au matumizi ya baadhi ya vidonge vya uzazi wa mpango.

Kutokana na sababu za ujauzito au matumizi ya vidonge vya uzazi wa mpango, melasma hutoweka baada ya mtoto kuzaliwa au mwanamke kuacha kutumia vidonge vya kupangilia uzazi.

Lakini pia melasma inaweza kudumu kwa kipindi kinachozidi hadi mwaka.

Na ikitokea imedumu kwa kipindi kirefu ni vyema kumuona daktari, ili kuppata tiba na inatibika.

Mwandishi wa makala haya ni daktari anapatikana kwa namba ya simu 0658 060 788