Upungufu wa damu kwa mjamzito unaweza kuzuiwa

Muktasari:

  • Hali hii husababisha uhitaji mkubwa wa madini ya chuma na virutubisho vya vitamini kwa ajili ya kutengeneza hemoglobin, moja ya vitu vinavyoiunda seli nyekundu kwenye damu.

Wakati wa ujauzito mabadiliko ya kiafya husababisha upungufu wa kiwango cha damu kwa asilimia 20 hadi 30.

Hali hii husababisha uhitaji mkubwa wa madini ya chuma na virutubisho vya vitamini kwa ajili ya kutengeneza hemoglobin, moja ya vitu vinavyoiunda seli nyekundu kwenye damu.

Upungufu huu wa damu ujulikanao kitaalamu ‘Anemia’ hujidhihirisha kwa mjamzito pale kiwango cha madini ya chuma kinachohitajika kuwa kikubwa ikilinganishwa na kilichopo.

Hali hii husababisha usafilishaji wa oksijeni kwenda sehemu mbalimbali za mwili kuwa hafifu.

Kuna aina ngapi za anemia

Kuna aina kuu tatu za anemia ambazo huwakumba wanawake kipindi cha ujauzito. Ya kwanza ni ya upungufu wa madini ya chuma.

Utafiti unaonyesha takribani wajawazito asilimia 15 hadi 25 hupatwa na aina hii ya anemia. Na wataalamu ya afya ya mama na mtoto wanasema madini hayo ya chuma husaidia usafirishaji wa oksijeni kutoka kwenye mapafu kwenda sehemu mbali mbali za mwili pamoja na kwa mtoto aliyeko tumboni.

Aina ya pili ni ya upungufu wa virutubisho vya vitamini aina ya foleti. Foleti hupatikana katika mboga za majani, malimao, ndizi, parachichi, machungwa, mapapai, maharagwe na karoti.

Kirutubisho hiki ni muhimu kwani husaidia kuujenga uti wa mgongo imara kwa mtoto aliyeko tumboni.

Aina ya tatu ni ya upungufu wa vitamini B12, ambayo ni muhimu kwenye uzalishaji wa chembe nyekundu za damu zenye kazi ya kusafirisha oksijeni kwa ajili ya kuupatia mwili nguvu.

Hata hivyo, tofauti na ukosekanaji wa aina hizo, kuna sababu nyingine huchangia upungufu wa damu.

Miongoni mwa sababu hizo ni pamoja na matatizo kwenye mfumo wa chakula unaosababisha kupoteza damu hasa kwa kipindi cha muda mrefu, nyingine ni maradhi kama malaria, Ukimwi, tatizo la seli mundu linalofahamika kwa jina la sikoseli, minyoo husabi ile inayonyonya damu katika mfumo wa chakula.

Je! Ni mambo gani yanayomuweka mjamzito katika hatari ya kupata upungufu wa damu?

Tunaambiwa miongoni mwa mambo yanayoweza kusababisha mjamzito kupata tatizo la upungufu wa damu ni pamoja na kubeba mimba zinazofuatana katika kipindi kifupi baada ya kujifungua, upungufu wa lishe yenye madini ya chuma, ujauzito wenye mapacha, kutokuwa na damu nyingi katika hedhi kabla ya ujauzito pamoja na kutapika sana wakati wa homa za asubuhi.

Namna unavyoweza kujitambua kuwa una tatizo hili

Tatizo hili la upungufu wa damu huambatana na dalili za maumivu ya kifua, kukabwa na pumzi, uchovu usio wa kawaida, maumivu ya kichwa hasa upande wa mbele, mapigo ya moyo kwenda haraka kwasababau katika kipindi hicho hemoglobin ya kusafirisha oksijeni mwilini huwa chache kutokana na upungufu wa madini ya chuma.

Hali hiyo husababisha moyo kupampu damu kwa haraka zaidi ili kuhakikisha oksijeni inasambaa katika sehemu mbalimbali za mwili kukidhi mahitaji, kupauka kwa ngozi na kucha, mikono na miguu kupatwa na ubadili, kutoweza kufikiria kwa makini, kwasababu ubongo unakuwa unahitaji oksijeni wakati wote.

Madhara yake

Madhara ya upungufu wa damu ni pamoja na kuongeza uwezekano wa kujifungua mtoto chini ya uzito wa kawaida, kuathiri ukuaji wa mtoto, matatizo katika ukuaji wa ubongo na uti wa mgongo, mimba kutoka kabla ya wakati, mtoto kupoteza maisha akiwa tumboni, uwezekano wa mama kupoteza maisha wakati wa kujifungua unaongezeka kama atapoteza damu nyingi wakati huo, husababisha pia matatizo ya moyo na mapafu na huongeza hatari ya kushambuliwa na maradhi mbalimbali.

Mambo ya kuzingatia kuepuka matatizo hayo

Wakati wa ujauzito ni muhimi kuhudhuria kliniki kwa ajili ya ushauri kutoka kwa daktari.

Kinga dhidi ya malaria ni ya muhimu kwani malaria ni moja ya chanzo cha anemia kwa wajawazito wengi. Pia kupata kinga dhidi ya minyoo, lishe bora inayojumuisha madini ya chuma ikiwamo nyama, kuku, samaki, mayai, maharagwe mboga za majani kama spinachi na vyakula vyenye vitamin C kama juisi ya machungwa inayosaidia unyonyaji wa madini ya chuma kutoka kwenye mfumo wa chakula kwenda kwenye damu.

Mjamzito anashauriwa anywe chai na kahawa ili kuzuia madini ya chuma kutoka kwenye mfumo wa chakula kwenda kwenye damu, hivyo inashauriwa asitumie kwa pamoja na vyakula vya madini ya chuma.

Dk Keneth ni daktari mwanafunzi anayepamba na kuepusha vifo vya mama na mtoto anapatikana kwa namba ya simu 0759 775788.