Zitambue dalili za sonana na matibabu yake

Muktasari:

  • Pamoja na sababu zinazochangia, lakini kitu kingine muhimu unachopaswa kukitambua ni dalili ugonjwa huo ni zipi.

Mwanamke mmoja kati ya watano na mwanaume mmoja kati ya 10 wamewahi kuugua sonona katika maisha yao. Takwimu hizi zinadhihirisha kuwa wanawake ndiyo waathirika wakubwa wa tatizo hilo.

“depression” ni neno la kisayansi ambalo kwa tafsiri ya kawaida ndiyo tunaita sonona. Huu ni ugonjwa wa akili ambao mtu anaupata baada ya kupitia matatizo fulani na kumuacha kwenye huzuni au kusononeka kwa muda mrefu. lakini watu wengi bado hawajui kama hali hiyo ni ugonjwa kama yalivyo maradhi mengine.

Pamoja na sababu zinazochangia, lakini kitu kingine muhimu unachopaswa kukitambua ni dalili ugonjwa huo ni zipi.

Ninapotathimini sonona nikiwa na mgonjwa, hua namuuliza maswali haya; kwa kipindi cha siku chache zilizopita, umeshawahi kupatwa na hali iliyokufanya ujione kama hauna thamani na kupoteza matumaini? Au unakosa hisia kwenye vitu ambavyo awali vilikua vinakupa furaha na amani?

Kama jibu la maswali haya ni “ndiyo”, basi ni dhahiri mgonjwa huyo anakuwa anaugua sonona. Dalili nyinginezo zinazopaswa kufuatiliwa ni pamoja na kukosa hamu ya kula, kukosa usingizi wa kutosha (aidha kuchelewa kulala au hata kuwahi kuamka), kushindwa kutilia maanani mambo muhimu, kujiona kama huna uwezo wa kufanya jambo fulani na kila unapopaswa kufanya jambo hilo, unahisi uchovu, lakini pia wakati mwingine mtu anashawishika kujinyonga.

Ni dhahiri kwamba sonona ni tishio la maisha, kutokana na ukweli kwamba husabisha mtu kutofurahia maisha yake binafsi.

Katika kufuatilia ni kwa kiasi gani mgonjwa ameweza kuathirika na sonona, madaktari hutumia njia ya mahojiano kati yake na mgonjwa. Njia hiyo kitaalamu inajulikana PHQ-9(Patient health questionnaire).

Kupitia njia hiyo, daktari humuuliza mgonjwa maswali tisa maalum ambayo majibu ya mgonjwa yataonyesha ni kwa kiasi gani ameathirika na sonona kabla ya kumfanyia vipimo.

Cha kusikitisha ni kwamba, waathirika wengi wa tatizo hilo huwa hawaendi kupata ushauri wa daktari kwa dhana ya kuona aibu au kuona kuwa sonona sio tatizo la kulitilia maanani.

Sonona ni ugojwa kama yalivyo maradhi mengine ambayo yanahitaji msaada na yasipopatiwa tiba, yanaweza kuleta madhara makubwa kwa maisha ya kila siku. Kwa mfano, kama mtu ana vidonda vya tumbo na huamua kuyadharau maumivu yanayoambatana na vidonda hivyo bila kupatia tiba, ukingo wa utumbo mpana unakua hatarini zaidi kuathirika na kulazimika kufanyiwa upasuaji.

Na kwa sonona ipo hivyo. Daktari huenda asikuambie “jizuie na sonona ina madhara” kama hautoonyesha kuhitaji msaada wa daktari, sonona ni zaidi ya uifikiriavyo. Itakufanya upoteze hisia na kushindwa kufurahia mambo yote ya kijamii ambayo kwa kawaida yanaleta furaha katika maisha ya kila siku.

Ikiwa mgonjwa hajaathirika sana na sonona, ushauri wa kisaikolojia kwa mgonjwa namna ya kukabiliana na tatizo, utamsaidia. Aidha, kwa mgonjwa ambaye ameathirika zaidi na tatizo hilo, tiba ya dawa italazimika kutolewa kwake.

“Antidepressants” ni jina la kitaalamu ambalo linajumuisha makundi ya dawa za kutibu sonona.

Hata hivyo, dawa hizi pia huwa zinaleta matokeo mengine baada ya kutumiwa kama zilivyo dawa za aina nyingine. Matokeo kama ya uchovu, kuharisha au kukosa haja, mdomo kukauka ni baadhi tu ya matokeo ya kawaida ambayo mgonjwa anayapata baada ya kuzitumia dawa hizo.

Lakini matokeo haya yanatoweka baada ya siku chache. Mgonjwa anapaswa kutumia dawa hizo kwa muda hata zaidi wa miezi sita na hatakiwi kuacha kuzitumia hata kama akianza kupata afadhali ili kupunguza uwezekano wa ugonjwa kujirudia tena.

Pia, ukiwa na sonona ni rahisi sana kusikia hali ya uchovu na kukosa ari ya kufanya chochote, unashauriwa ufanye mazoezi kwani yanasaidia kusisimua vichocheo vinavyoleta hisia za kujisikia vizuri.

Hivyo ni muhimu kujilazimisha kufanya mazoezi hata kama unahisi uchovu.