
| Wizara:Msisubiri Tanesco tumieni umeme jua | Send to a friend |
| Saturday, 04 February 2012 08:37 |
|
WIZARA ya Nishati na Madini imesema kuwa itaendelea kuunga mkono juhudui za usambazaji umeme wa mionzi ya jua kwa wananchi ikiwataka wananchi hao hasa wa vijijini kutosubiri umeme wa Tanesco, badala yake watumie umeme huo. Kauli hiyo imetolewa na Kamishna wa Nishati na Petroli wa wizara hiyo, Theophilo Bwekea jijini Dar es Salaam jana, katika maonyesho ya bidhaa na vifaa vya umeme jua yaliyoandaliwa na Kampuni ya Ensol sanjari na kampuni hiyo kutimiza miaka kumi. Bwekea alikuwa mgeni rasmi katika maonyesho hayo kwa niaba ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini, Eliakim Maswi. “Wito wangu wananchi wasisubiri umeme wa Tanesco, watumie umeme jua kwani ni rahisi na hauna mizengwe, unaleta maendelero. Serikali itaendelea kuisaidia Ensol ii umeme jua uende vijijini, “alisema Bwekea. Alifafanua kuwa wizara yake itaendelea kuisaidia sekta ya umeme jua kwa kuboresha sera zake, misamaha ya kodi kwa bidhaa za umeme jua na kutoa bure mafunzo ili kuwezesha asilimia 30 ya Watanzania kufikiwa na umeme ifikapo mwaka 2015. Alisema uenezaji wa teknolojia ya umeme wa nguvu ya mionzi ya jua unaweza kupewa msukumo zaidi na sekta binafsi na kueleza kwamba Serikali pia inaweka msukumo kuhakikisha umeme jua unawafikia Watanzania wengi zaidi. Naye Mkurugenzi mtendaji wa Ensol Khamis Mikate alisema kuwa sekta hiyo ina changamoto mbalimbali ikiwamo uingizwaji wa vifaa bandia wa vifaa bandia vya umeme jua na kukosekana mafundi wa kutosha. Hata hivyo alisema kuwa bei ya vifaa vya umeme jua itashuka katika mwaka huu kutokana na bei hiyo kushuka pia katika Soko la Dunia na kwamba kampuni yake itaendleas kutoa mafuzo zaidi kuhusu umeme jua ili wataalamu waongezeke na kufikisha umeme jua kwa wananchi wengi zaidi. |














