
| Wafugaji watakiwa kujenga nyumba bora | Send to a friend |
| Thursday, 02 September 2010 22:01 |
|
SERIKALI imeombwa kuwahamasisha wananchi wa jamii za wafugaji kujenga nyumba za kudumu ili kuwa na makazi maalumu, na kuachana na utamaduni wao wa kuhamahama. Ilielezwa kuwa kama jamii hizo zitahamasishwa na kuelewa umuhimu wa kuwa na nyumba za kisasa katika makazi yao, wataacha tabia ya kuhamahama. Ushauri huo ulitolewa juzi na Mwenyekiti wa Serikali ya Kitongoji cha Losioi kilichopo katika Kijiji cha Kwamwande, wilayani Kilindi, Paulo Parasino, wakati akitoa maoni yake katika mkutano wa hadhara wa kutoa elimu ya afya hasa ya uzazi kwa njia ya sinema. Mkutano huo uliwakutanisha wakazi wengi wa eneo hilo baada ya kuandaliwa na Shirika la Utafiti na Tiba barani Afrika kupitia Mradi wake wa afya ya uzazi kwa vijana wa jamii za kifugaji unaotekelezwa kwa kushirikiana na Halmashauri ya Wilaya ya Kilindi "Naomba nitumie nafasi hii kuishukuru Serikali kupitia Shirika la Amref kwa kuweza kutuletea elimu hii hapa kwetu. Hii ni mara ya kwanza kupata semina kama hii kupitia sinema ambayo imefanya watu kufurahi na kuwa huru kuchangia kwa kutoa maoni yao'' alisema Parasino na kuongeza. Jamii yetu ya wafugaji hasa sisi wamasai tumekuwa nyuma kimaendeleo kutokana na kukosa elimu. Lakini hii inatokana na tabia ya kuhamahama, hii inatokana na kutojenga nyumba za kudumu ndiyo maana leo yupo Kilindi kesho Handeni. Naiomba Serikali ihamasishe jamii hizi za wafugaji ili wajenge makazi ya kudumu na kufanya waweze kuelimika na kupata fursa sawasawa na jamii nyingine zinazotuzunguka,'' alisema mwenyekiti huyo. Mwenyekiti huyo alisema jamii hiyo inakabiliwa na tatizo la kukumbatia mila zilizopitwa na wakati ikiwemo ukeketaji na kuwaoza mabinti wao mapema ili wajipatie mali. |













