
| Sumatra yapata Sh 14 milioni kwa madereva wazembe | Send to a friend |
| Thursday, 02 September 2010 22:11 |
|
MAMLAKA ya Udhibiti wa Usafiri wa Nchi Kavu na Majini (Sumatra), Kanda Nyanda za Juu Kusini imepata Sh 14 milioni za faini kutokana na makosa mbalimbali ya madereva wanaokiuka taratibu. Mkurugenzi wa Sumatra kanda hiyo, Amani Shamaje alisema fedha hizo zilikusanywa katika kipindi cha mwezi wa Mei mwaka huu pekee katika operesheni iliyofanyika mkoani Mbeya kuwabana madereva wanaokiuka taratibu za usafirishaji”. Shamaje alisema katika operesheni hiyo magari zaidi ya 50 yalikutwa na makosa ya uvunjaji wa sheria za usafirishaji na kwamba faini kwa kila gari ilikuwa Sh 250,000. Akizungumzia kuendelea kwa operesheni hiyo, alisema katika kipindi hiki cha kampeni za uchaguzi wa madiwani, wabunge na Urais, Sumatra kanda hiyo imeamua kusitisha kazi hiyo kutokana polisi kujikita zaidi katika kusimamia suala la usalama wa wagombea hao na wananchi. “Ni suala la ustaarabu tu, huwezi ukaanza kuwakamata madereva wanaovunja sheria hizo na hasa ukizingatia uchaguzi mkuu unagusa maisha ya watu, hivyo ili kuepusha vurugu zisizo na msingi ni vema tukaacha mpaka mwezi Novemba mwaka huu, mambo ya uchaguzi yatakapokuwa yamekwisha” alisema. Hata hivyo alitoa wito kwa madereva kuacha mra moja kuvunja sheria za barabarani na kwamba wavunjaji watachukuliwa hatua za mara moja watakapobainika. |













