Acacia yasaka ubia na wawekezaji wengine

Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini, Profesa Simon Msanjila


Muktasari:

  • Taarifa ya kampuni hiyo imetolewa baada ya vyombo vya habari vya kimataifa kuripoti kuwa inafanya mazungumzo na mwekezaji kutoka China kwa ajili ya kuingia ubia wa kibiashara.

Dar es Salaam. Kampuni ya uchimbaji madini ya Acacia imeanza mazungumzo na wawekezaji mbalimbali kwa ajili ya kuingia ubia kwenye miradi yake. Acacia ambayo inamiliki migodi ya Buzwagi, Bulyanhulu na North Mara ilisema kwenye taarifa yake jana kuwa, mazungumzo hayo ni ya awali na si rasmi.

Taarifa ya kampuni hiyo imetolewa baada ya vyombo vya habari vya kimataifa kuripoti kuwa inafanya mazungumzo na mwekezaji kutoka China kwa ajili ya kuingia ubia wa kibiashara.

Pia, kumekuwepo na tetesi kuwa wawekezaji hao wa China wameanza kutembelea migodi inayomilikiwa na kampuni hiyo kwa ajili ya kutathmini kabla la kuingia ubia.

Kwa mujibu wa ufafanuzi huo Acacia imekubali kuwepo kwa wawekezaji hao lakini wapo katika hatua za awali na hakuna uhakika kama makubaliano yatafikiwa.

Akizungumza kuhusu ubia huo, Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini, Profesa Simon Msanjila alisema Acacia wapo huru kuuza kampuni yao au vitega uchumi vyao kwa kufuata sheria.