DTB yaahidi neema

Muktasari:

  • Ahadi hiyo imetolewa na meneja wa benki hiyo, Viju Cherian kwa wajasiriamali hao kwenye warsha iliyofanyika mjini Morogoro jana.

 Benki ya Diamond Trust (DTB) imewaahidi wajasiriamali wadogo na kati kuwapatia mkopo Sh500 milioni ndani ya siku tano.

Ahadi hiyo imetolewa na meneja wa benki hiyo, Viju Cherian kwa wajasiriamali hao kwenye warsha iliyofanyika mjini Morogoro jana.

“Kutokana na mchango wao kwenye uchumi, wajasiriamali wadogo na kati wanahitaji kuungwa mkono kwenye shughuli zao. Kwa miaka miwili iliyopita, tumekopesha zaidi ya Sh285 bilioni. Kwa sasa, mteja anaweza kupata mpaka Sh500 milioni ndani ya siku tano tu,” alisema Cherian kwenye warsha hiyo ya kuwajengea uwezo wajasiriamali.

Kwa kushirikiana Kampuni ya Ushauri wa Kodi ya PFK Associates, wajasiriamali walifundishwa namna ya kutunza vitabu vya kumbukumbu za biashara, Sheria ya Kodi na utaratibu wa kulipa, Sheria ya Fedha ya mwaka 2017 pamoja na Sheria ya Ajira.

Fursa hiyo pia, ilitumika kuwapa uelewa wa bidhaa mbalimbali zinazotolewa na benki hiyo pamoja na taasisi nyingine za fedha kama udhamini wa benki kwenye miradi mikubwa, udhamini wa bima na uhamishaji wa fedha.

Cherian alisema wafanyabiashara hao wanahitaji kuboresha mazingira yao hasa kuzingatia sheria na kanuni za nchi ili kusonga mbele zaidi.