Mauzo soko la hisa yazidi kuporomoka

Muktasari:

Takwimu za DSE zinaonyesha wiki iliyoishia Septemba 22, mauzo ya soko hilo yalikuwa Sh53 bilioni ambayo yalipungua kwa Sh50 bilioni Septemba 29. Kutoka Sh3 bilioni za Septemba 29, wiki iliyoishia Oktoba 6 mauzo yameshuka kwa nusu na kufikia Sh1.5 bilioni.

Dar es Salaam. Mauzo ya Soko la Hisa la Dar es Salaam (DSE), yameendelea kupungua hadi Sh1.5 bilioni Oktoba 6, kwa wiki ya pili sasa.

Takwimu za DSE zinaonyesha wiki iliyoishia Septemba 22, mauzo ya soko hilo yalikuwa Sh53 bilioni ambayo yalipungua kwa Sh50 bilioni Septemba 29. Kutoka Sh3 bilioni za Septemba 29, wiki iliyoishia Oktoba 6 mauzo yameshuka kwa nusu na kufikia Sh1.5 bilioni.

Mkurugenzi wa Kampuni ya Orbit Securities, Simon Juventus alisema kupungua kwa mauzo hayo ni kwa sababu wawekezaji wanalitazama soko kwanza kuona namna wanavyoweza kufaidika kama lilivyo lengo la wafanyabiashara wote.

Licha ya mauzo, idadi ya hisa zilizouzwa na kununuliwa imepungua kutoka 800,000 Septemba 29 hadi 600,000 Oktoba 6.

Hata hivyo, ukubwa wa mtaji wa kampuni zilizoorodheshwa sokoni hapo umeongezeka kwa Sh431 bilioni kutoka Sh20.3 trilioni wiki iliyoishia Septemba 29 hadi Sh20.8 trilioni. Ongezeko hilo linatajwa kutokana na kupanda kwa bei ya hisa za Kampuni ya Acacia kutoka Sh4,980 hadi Sh5,710, Vodacom kutoka Sh770 hadi Sh850, Nation Media Group (NMG) kutoka Sh2,360 hadi Sh2,390.

Juventus alisema hisa za Vodacom zinapanda kwa sababu watu wana imani na kampuni hiyo kwa matarajio kuwa itafikia malengo yake na wao watapata gawio wanalotarajia.