Mbio za mlima K’njaro kuchochea utalii nchini

Muktasari:

  • Katika mbio hizo zitakazoanzia katika kilele cha Uhuru na kuishia geti la Marangu, watalii kumi ndiyo watakaoshiriki kati ya 17 waliopanda mlima jana.

        Moshi. Mbio za Kilimanjaro Extreme zinazotarajiwa kufanyika Desemba 9 mwaka huu katika kilele cha mlima Kilimanjaro, zimeelezwa kuwa zitaongeza idadi ya watalii nchini.

Katika mbio hizo zitakazoanzia katika kilele cha Uhuru na kuishia geti la Marangu, watalii kumi ndiyo watakaoshiriki kati ya 17 waliopanda mlima jana.

Mkurugenzi wa Kampuni ya Eaongoza Watalii (Killsmile trails of safari Limited), iliyoandaa mbio hizo, Hamadi Hasan alisema lengo ni kuongeza pato la Taifa kupitia watalii.

Hasan alisema washiriki wa mbio hizo watatumia saa nne hadi nane kutoka kilele cha Uhuru hadi kufika geti la Marangu.

Michael Gowron, ambaye ni mshirika wa maandalizi ya mbio hizo alisema uandaaji umechukua miaka miwili kutokana na kufatilia vibali kutoka kwa wahusika na Serikali.

Ofisa wa kitengo cha utalii, Hifadhi ya mlima Kilimanjaro, Charles Ng’endo alisema hiyo ni aina mpya ya utalii kwa wanamichezo na watu wengine. (Zainab Maeda)