Mwijage: CBE toeni elimu ya ujasiriamali

Muktasari:

  • Akizindua bodi ya CBE jana, Mwijage alisema ujasiriamali liwe somo la lazima ili kukabiliana na tatizo la ukosefu wa ajira.

Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Charles Mwijage ameutaka uongozi wa Chuo cha Elimu ya Biashara (CBE) kutoa elimu ya ujasiriamali ili wahitimu waweze kujiajiri.

Akizindua bodi ya CBE jana, Mwijage alisema ujasiriamali liwe somo la lazima ili kukabiliana na tatizo la ukosefu wa ajira.

“Katika zama hizi na tunakokwenda, kuajiriwa itakuwa zilipendwa, hivyo tuwafundishe vijana ili wawe na uwezo wa kuajiriwa na kujiajiri,” alisema Mwijage.

Alifafanua kuwa zamani wahitimu wa vyuo vikuu walitegemea ajira za Serikali lakini sasa hali iko tofauti.

Mwijage alisema chuo hicho kinatakiwa kutoa elimu itakayowasaidia kuwa na mbinu nyingi za ubunifu na kujiajiri.

Mwenyekiti mpya wa bodi, Ester Ishengoma alimhakikishia waziri kuwa bodi hiyo inafuata maelekezo yake kwa lengo la kukiboresha chuo hicho.

(Raymond Kaminyoge)