NMB kuanza kutoa mikopo ya nyumba

Mkuu wa kitengo cha mauzo wa Benki ya NMB, Omari Mtiga akizungumza wakati wa mkutano na wanahabari jijini Dar es Salaam juzi. Kulia ni meneja mikopo ya nyumba, Miranda Lutege na Kushoto ni meneja mwandamizi wa wateja binafsi, Ally Ngingite. Picha na Omari Fungo

Muktasari:

Taarifa ya benki hiyo inasema wanufaika watakuwa Watanzania wanaoishi nchini hata ughaibuni wanaotaka ama kununua, kujenga au kukarabati.

Dar es Salaam. Benki ya NMB imezindua mikopo ya nyumba itakayolipwa kwa riba nafuu ndani ya miaka 15.

Taarifa ya benki hiyo inasema wanufaika watakuwa Watanzania wanaoishi nchini hata ughaibuni wanaotaka ama kununua, kujenga au kukarabati.

Meneja wa mikopo ya nyumba wa NMB, Miranda Lutege alisema mteja aliyekidhi vigezo atapewa asilimia 80 ya thamani ya nyumba anayotaka kujenga, kukarabati au kununua.

“Kiwango cha juu cha mkopo kwa mteja ni Sh700 milioni. Mume na mke wanaweza kuunganisha kipato chao na kupewa mkopo huu kukamilisha ndoto yao ya kumiliki nyumba,” alisema Lutege.

Naye mkuu wa kitengo cha mauzo kwa wateja, Omary Mtiga alisema kabla ya kuuchukua mkopo utakaorejeshwa ndani ya miaka 15, mteja atatakiwa kuweka asilimia 10 ya kiwango anachoomba.

Kigezo muhimu cha mkopo huo ni muombaji kuwa na hatimiliki ya nyumba au kiwanja anachotaka kujenga nyumba.