Walionunua Sumsung Galaxy Note 7 kurudishiwa gharama zao

Muktasari:

Hatua hiyo imefuata baada ya kubainika kwamba simu hizo ni hatari kwa sababu betri zake zinalipuka. Tanzania ni miongoni mwa nchi zilizopiga marufuku uingizaji wa simu hizo nchini kwa sababu za kiusalama.

Dar es Salaam. Kampuni ya Sumsung Afrika Mashariki (SEEA) imetangaza kuwabadilishia simu au kuwarudishia gharama zao wateja wote walionunua simu za Samsung Galaxy Note 7 popote duniani.

Hatua hiyo imefuata baada ya kubainika kwamba simu hizo ni hatari kwa sababu betri zake zinalipuka. Tanzania ni miongoni mwa nchi zilizopiga marufuku uingizaji wa simu hizo nchini kwa sababu za kiusalama.

Kwa mujibu wa tangazo lililotolewa kwenye vyombo vya habari, watu walionunua simu hizo watabadilishiwa na kupewa simu ya Galaxy S7 au Galaxy S7 Edge au Galaxy Note 5 na watarudishiwa gharama za ziada.

Mbali na kuwabadilishia simu, kampuni hiyo imefafanua kwamba wateja wanaotaka kupewa fedha taslimu watarudishiwa fedha kamili walizonunulia Samsung Galaxy Note 7 kama wana uthibitisho wa risiti.